Na RICHARD MUNGUTI
ALIYEKUWA waziri wa Michezo na Jinsia, Dkt Hassan Wario huenda akasukumwa jela miaka 10 baada ya kupatikana na hatia ya matumizi mabaya ya pesa zilizotengewa wanariadha walioshiriki Michezo ya Olimpiki ya Rio de Janeiro nchini Brazil 2016.
Wario alipatikana na hatia ya kutumia mamlaka ya afisi yake vibaya na kufuja pesa ambazo zingaliwafaidi wanamichezo.Hakimu mkuu wa mahakama ya kuamua kesi za Ufisadi, Bi Elizabeth Juma, alisema kashfa hiyo ilipelekea zaidi ya Sh55 milioni kupotea.
Wario pamoja na aliyekuwa afisa mkuu wa Kamati ya Olimpiki Kenya (Noc-K) Stephen arap Soi, pia watatozwa faini maradufu ya pesa zinazodaiwa kufujwa.
Wario alipatikana na hatia katika mashtaka matatu. Naye Soi alipatikana na hatia katika mashtaka sita.Wote wawili watajua hatima yao leo, mahakama itakapopitisha hukumu hiyo.
Katika uamuzi uliosomwa kwa muda wa saa tano, hakimu mkuu Bi Juma alisema Wario alitumia mamlaka ya afisi yake vibaya. Aliwapa pesa watu ambao hawakuwa katika orodha ya waliopaswa kusafiri hadi Rio de Janeiro mnamo Julai 2016.
Waliofaidi na ufisadi huo walitajwa kuwa Adan Omar Enow, Richard Abura na Monica Sairo.Soi alipatikana na hatia ya kutofuata mwongozo na utaratibu uliowekwa na sheria ya usimamizi wa pesa za umma.
Hakimu alisema mashahidi 22 walioitwa na upande wa mashtaka, walithibitisha jinsi msimamizi huyo wa timu iliyowakilisha Kenya katika michezo hiyo aliidhinisha matumizi ya Dola za Marekani 151,500 kama marupurupu kwa washiriki wa michezo hiyo.Pia alishtakiwa kwa kusababisha kupotea kwa Sh9.7 milioni.
Pia mahakama ilisema Soi alisababisha kununuliwa kwa tikiti za ndege za thamani ya Sh19.5 milioni na akalipa watu wengine Sh4.9 milioni.