• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 10:08 PM
Jambojet yazindua safari za Lamu

Jambojet yazindua safari za Lamu

NA KALUME KAZUNGU

KAMPUNI ya ndege ya Jambojet kwa mara nyingine imezindua safari zake kwenye anga ya Lamu baada ya kuzikatiza kwa karibu miaka mitano iliyopita.

Mnamo 2015, kampuni hiyo ilizindua safari zake Lamu lakini ikazikatiza 2017 kwa kile walichodai kuwa ni ukosefu wa usalama na pia hali mbaya ya uwanja wa ndege wa Manda eneo hilo.

Aidha hafla ya kuzindua upya safari za ndege ya Jambojet iliandaliwa Jumatano uwanjani Manda na kuhudhuriwa na Waziri wa Utalii na Wanyamapori, Najib Balala, makatibu wa Wizara za Utalii na Uchukuzi, wakuu wa kampuni ya Jambojet miongoni mwa maafisa wengine wakuu serikalini.

Akihutubu kwenye sherehe hiyo, Bw Balala alitaja kurejelewa kwa safari za ndege ya Jambojet Lamu kuwa mwamko mpya kwa sekta ya utalii Lamu.

Bw Balala aliiomba Wizara ya Uchukuzi na Mamlaka ya Usimamizi wa Viwanja vya Ndege nchini (KAA) kuharakisha ujenzi na uboreshaji wa uwanja wa ndege wa Manda unaoendelea kwa sasa ili kuuwezesha kupokea ndege zaidi za wageni na watalii wanaozuru Lamu.

Aliisifu serikali kuu kwa juhudi ilizofanya kukabiliana na magaidi wa Al-Shabaab na kuimarisha usalama Lamu.

Alisema ana matumaini kwamba msimu wa juu wa utalii utakapoanza Disemba mwaka huu utavutia watalii wengi kuja Lamu,ikizingatiwa kuwa eneo hilo limeshuhudia usalama wa hali ya juu miaka ya hivi sasa.

“Tunashukuru kwamba Jambojet wamerejelea safari zake Lamu. Huu ni mwamko mpya kwa sekta ya utalii. Natumai KAA itafanya bidi kukamilisha ukarabati unaoendelea wa kiwanja cha Ndege cha Manda kabla msimu wa wageni wengi Disemba ufike,” akasema Bw Balala.

Afisa Mkuu Mtendaji na Meneja wa Jambojet nchini, Karanja Ndegwa alisema hatua yao ya kurejelea safari za Lamu inatokana hasa na kuimarika kwa usalama Lam una pia kuboreshwa kwa uwanja wa Ndege wa Manda.

Bw Ndegwa alisema nauli ya kutoka Nairobi hadi Lamu itakuwa Sh7,100 ilhali ilhali ile ya Mombasa hadi Lamu ikitozwa Sh4,600.

Alisema watakuwa wakitekeleza safari mara nne eneo la Lamu kila wiki.

Alisema kampuni ya Jambojet iliafikia kuzindua safari ya Lamu kutokana na kwamba eneo hilo ni muhimu kwa watalii hapa nchini.

“Kuzinduliwa kwa mradi kama vile Bandari ya Lamu (Lapsset) kutavutia wasafiri na wawekezaji wengi kuja Lamu. Tunataka kurahisisha usafiri waokupitia ndege nah ii ndiyo sababu tukaafikia kurejesha safari zetu hapa,” akasema Bw Ndegwa.

Afisa huyo alisema juma lililopita, Jambojet pia ilizindua safari zake eneo la Goma huko Demokrasia ya Congo (DRC)

Kwa upande wake,Gavana wa Lamu, Fahim Twaha aliomba kampuni nyingi zaidi za ndege kuzindua safari zake za Lamu, akitaja kuwa eneo hilo linafurahikia usalama.

You can share this post!

Madereva Wahome, Hamza na Kimathi kupeperusha bendera ya...

ULIMBWENDE: Maji ya mchele yana faida nyingi kwenye ngozi...