Na RICHARD MUNGUTI
WATENGENEZAJI wawili wa pombe kali wameshtakiwa kwa kupatikana na Ethanol yenye thamani ya Sh53milioni.
Ethanol hii inayotumika kutengeneza pombe kali haikuwa imelipiwa ushuru.Mabw Martin Ng’ang’a na Julius Njoroge Mburu walikanusha shtaka hilo waliposhtakiwa mbele ya hakimu mkuu mahakama ya Milimani Bw Francis Andayi.
Mahakama ilifahamishwa na kiongozi wa mashtaka Bi Angela FuchakaMnamo Septemba 7, 2021 katika kiwanda cha Viken Thirty Industrial Park kilichoko eneo la Ruai Nairobi wawili hao walikutwa wanahifadhi Ethanol lita 153,580.50.
Ethanol hii ilikuwa imehifadhiwa ndani ya mapipa 618 250.Maafisa wa polisi na wale kutoka idara ya ushuru (KRA) walikamata ethanol hiyo yenye thamani ya Sh 53,737,580.
Washtakiwa hao kupitia wakili wao waliomba mahakama iwaachilie kwa dhamana wakisema makazi yao yanajulikana na hawawezi toroka.Bi Fuchaka hakupinga washtakiwa wakiwachiliwa kwa dhamana.
“Nimetilia maanani ombi la washtakiwa kuachiliwa kwa dhamana na kwamba upande wa mashtaka haupingi dhamana,”alisema Bw Andayi.Kila mmoja wao alipewa dhamana ya Sh 500,000 pesa tasilimu.