• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 12:58 PM
Raila tosha 2022, Joho asema

Raila tosha 2022, Joho asema

Na WINNIE ATIENO

GAVANA wa Mombasa Hassan Joho ametupilia mbali azma yake ya kuwania urais na kuamua kuunga mkono azma ya kiongozi wa ODM Raila Odinga.

Bw Joho amesema analenga kuhakikisha kuwa eneo la Pwani linapata uwakilishi kamili katika serikali ijayo.Gavana huyo wa Mombasa jana aliwataka viongozi wa pwani kuunga kwa lengo la kuhakikisha kuwa Chama cha Uniteda Democratic Alliance (UDA) kinachohusishwa na Naibu Rais William Ruto hakivurugi umoja wa eneo la pwani kisiasa.

Wakati huu ndoto urais ya Dkt Ruto inaungwa mkono na wabunge wawili pekee waliochaguliwa kwa tiketi ya ODM. Wao ni mbunge wa Malindi Aisha Jumwa na mwenzake wa Kinango Benjamin Tayari.

Viongozi wa Pwani waliokutana na Bw Odinga jana mjini Mombasa walisema wataunga kwa ajili ya kuhakikisha kuwa Pwani inanufaika katika serikali ijayo.

Gavana Joho, Granton Samboja (Gavana wa Taita Taveta), Dhadho Godana (Gavana wa Tana River) na wabunge Omar Mwinyi (Changamwe), Badi Twalib (Jomvu), Zulekha Hassan (Mbunge Mwakilishi wa Kwale), Asha Hussein (Mbunge Mwakilishi, Mombasa), Ali Wario (Garsen), Teddy Mwambire (Ganze), Ken Chonga (Kilifi Kusini) na mfanyabiashara wa Mombasa Suleiman Shabhal walitangaza kuwa wanaounga mkono azma ya Bw Odinga kuingia Ikulu.

Walifanya hivyo kupitia kile walichokitaja kama Azimio la Pwani.Bw Mung’aru ambaye anataka kuwania kiti cha ugavana wa Kilifi alimshukuru Rais Uhuru Kenyatta kwa kutekeleza miradi mingi ya maendeleo eneo la Pwani.Gavana Joho ambaye anahudumu muhula wake wa pili na wa mwisho alisema kuwa haogopi kustaafu.

Alisema eneo la Pwani litaweza kusuluhisha changamoto zake kama vile za kiuchumi na dhuluma katika umiliki wa ardhi kwa kuwa ndani ya serikali ijayo.

“Wakati huu, pwani haitaki uungwaji bali ushirikiano. Katika kinyang’anyiro cha urais, ikiwa sio Odinga ni Joho. Hatutaki kujiweka katika hali ambapo kila mwaka tunaomba kana kwamba sisi sio Wakenya halisi. Bw Odinga aliunda baraza lake la mawaziri tutakuwa serikalini kisheria wala sio kama waalikwa,” Bw Joho akasema.

You can share this post!

Serikali kugawana malipo na wauguzi wanaotumwa UK

CBC: Onyo wazazi wasifanyie watoto kazi za ziada