• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
KINA CHA FIKIRA: Asilan usimchape na kumtesa punda akubebeaye mizigo

KINA CHA FIKIRA: Asilan usimchape na kumtesa punda akubebeaye mizigo

Na WALLAH BIN WALLAH

WAJIBU wa wanadamu ni kufaana na kusaidiana katika kuishi.

Unifae nikufae; unisaidie nikusaidie.

Huo ndio utu na uungwana kwa watu wenye hekima na busara isiyoleta hasara maishani. Hekima na busara husaidia sana katika utekelezaji wajibu kuboresha maisha duniani.

Kwa hakika binadamu tumeumbwa kufaana wala si kufanana!

Tunaishi kwa kutegemeana na kuegemeana kama mafya au mafiga ya mekoni ndipo tupate mafanikio! Kila mtu anahitaji ushirikiano wa mwenzake katika kuishi.

Mara nyingine, hutokea mwanadamu akahitaji huduma na uwezo wa wanyama wengine pia ili kuwasaidia kufanya kazi.

Viongozi wa serikali nchini huhitaji juhudi za raia au wananchi wachapakazi wajitoleao kujenga taifa lipate maendeleo.

Taifa lisilokuwa na wananchi wachapakazi haliwezi kuendelea! Raia ndio watumishi wa kuitumikia nchi.

Ni bora watunzwe vyema na wahudumiwe vizuri kwa kuwa wao ndio wamejitwisha na kutwishwa mizigo ya kuijenga nchi. Wananchi ndio nguvukazi na uti wa mgongo wa uchumi wa taifa.

Kwa hivyo, wasiteswe wala kunyanyaswa kulihali!!Wakuu na waajiri wote wenye miradi ya uzalishaji mali huhitaji wafanyakazi wa kuwasaidia kuinua viwango vya mapato kazini.

Kampuni zote au mashirika na viwanda vya uchumi na biashara huwategemea pakubwa wafanyakazi wao!

Mwajiri na mwajiriwa, wote wanafaana na kutegemeana sawasawa kama sahani na kawa katika kuleta faida kazini.

Muhimu tuelewe kwamba mfanyakazi si mtu duni. Bila huyo mfanyakazi, kazi haifanyiki! Mwajiri naye asipokuwapo, mwajiriwa hana kazi. Lakini mwajiri hawi mtenda yote bila nguvu za mfanyakazi!

Mkondo huu wa kutumikiwa na kutumikia ndio unaoitwa kutumikiana au kufaana!

Mtumikiwa asimpuuze na kumnyanyasa mtumikiaji kwa kumchukulia kuwa ni punda mbeba mizigo tu! Mara nyingi Babu yangu Mzee Majuto aliniambia, ‘Mjukuu wangu, mtu yeyote anayekusaidia kufanya kazi ya kuzalisha mali, anakuongezea mchango adhimu na ufanisi katika kukuza mali yako! Umtunze vizuri kwa mchango wake wa kukusaidia kufanya kazi. Wafanyakazi wowote wale: walimu, wakulima, wavuvi, askari, madaktari, mawakili, madereva, waandishi, wanahabari, wachuuzi, marubani, wapagazi, matopasi na wengineo ni wadau wakuu wa kuzalisha mali na kuboresha uchumi nchini! Watukuzwe!’

Ndugu wapenzi, mtu yeyote anayekufanyia kazi, anakusaidia kubeba mzigo wa uchumi na maendeleo!

Mtu huyo ni sawa na punda ambaye amekubebea mizigo mizito ya mali ambayo labda usingebeba peke yako! Umheshimu! Usimpige! Umlipe vizuri na kumtunza tu! Usimnyanyase! Usimtese na kumchapa punda anayekubebea mizigo! Unamchapia nini ilhali amekusaidia kukubebea mizigo????

You can share this post!

Fisi aibiwa tairi akila vya haramu

SAUTI YA MKEREKETWA: Wizara sasa ifanye uamuzi imara kuhusu...