• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 10:08 PM
TAHARIRI: Sarakasi hazimfai raia anayeumizwa

TAHARIRI: Sarakasi hazimfai raia anayeumizwa

KITENGO CHA UHARIRI

WANANCHI wanapoendelea kuumizwa na bei ya juu ya mafuta, kila mtu anajaribu kujiondolea lawama.

Maseneta, kwa kutaka kujipendekeza kwa wapigakura, jana Jumanne walijaribu kufurahisha umma kwa kutaka kuwahoji mawaziri wawili. Mawaziri hao John Munyes (Petroli) na Charles Keter (Kawi) walipuuza mwaliko huo.

Spika wa Bunge la Kitaifa Justin Muturi, ambaye aliongoza Bunge mwaka 2018 kupitisha Mswada wa Fedha, safari hii amejitokeza kuwa mkosoaji.

Akizungumza wikendi eneo la Runyenjes, Embu, Bw Muturi aliwataka wabunge wawasilishe bungeni marekebisho ya sheria hiyo.Siku walipopitisha, Bw Muturi alionekana kusukuma wabunge waharakishe shughuli hiyo, bila kusikiza waliokuwa na pingamizi.

Maseneta, kwa kutaka kujipendekeza kwa wananchi, walichukua jukumu lisilo lao. Waliwaita mawaziri kujadili kuhusu Sheria ya Fedha (2018), ambayo ushuru uliopendekezwa umeanza kuonekana athari yake.

Wakenya wanapopambana na ugumu wa maisha kutokana na janga la Corona, ipo haja ya kuangalia upya sheria hiyo. Kwa sababu ya ushuru kupita kiasi kwenye bei ya mafuta, bidhaa hiyo ni ghali humu nchini kuliko ilivyo Uganda.

Taifa lisilokuwa na bandari, linalotoa mafuta yake kwenye bandari ya Mombasa na kuyapitishia nchini, linauza lita moja ya petroli Sh4300 za Uganda, sawa na Sh131 za Kenya.

Hiyo ndiyo bei ya juu zaidi Uganda, ikilinganishwa na Sh147 mjini Mandera.

Maseneta wanafahamu kwamba Katiba inalipatia Bunge la Taifa jukumu na mamlaka ya kuhusika na masuala ya fedha. Mswada uliopandisha ushuru wa mafuta unaweza tu kurekebishwa na wabunge.

Si maseneta wala mawaziri.

Ndio maana mawaziri Munyes na Keter ambao ni maseneta wa zamani, walikataa kufika mbele ya Seneti.

Walijua mwaliko huo ni sarakasi tupu.

Ingawa Jaji wa Mahakama Kuu George Odunga aliamua kwamba sheria hiyo ya ushuru ni batili, Serikali imeonyesha siku za nyuma kuwa haiheshimu maamuzi ya korti.

Kinachohitajika sasa ni mbunge yeyote kuunda mswada wa marekebisho ya sheria hiyo.

Mswada huo ujadiliwe kwa haraka na kuondoa sheria inayotoza ushuru zaidi kwa mafuta.

Bila hivyo, agizo la Spika kwamba Kamati ya Fedha ichukue wiki mbili kuangalia suala hilo, ni sarakasi isiyowaondolea dhiki wananchi.

You can share this post!

Simiyu atumai Oluoch, Keyoga watapona kabla ya Edmonton 7s...

Bei ya mafuta: Kioni asisitiza wabunge ndio wa kulaumiwa