• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 1:08 PM
TAHARIRI: TSC idhibiti zogo la shule haraka

TAHARIRI: TSC idhibiti zogo la shule haraka

KITENGO CHA UHARIRI

RIPOTI kuhusu uchomaji wa shule kubwa za upili humu nchini siku mbili zilizopita zinaibua hofu kuu kwa wazazi hasa ikikumbukwa kwamba mwaka huu wa masomo ni mfupi mno na wanafunzi, walimu wana kazi nyingi kukamilisha kabla ya Machi 2022.

Kando na miaka ya awali, wadau sasa wanahitajika kusomesha silebasi ya mwaka mzima katika wakati mfupi uliowekwa na wizara ya Elimu.

Katika hali hii, shule zinafaa kuwa na mazingira matulivu yatakayoyawezesha kufikia maazimio na malengo yao kimasomo, kama kupasi mitihani ijayo kwa alama za juu.

Serikali, walimu, wazazi, wanafunzi na wadau wote katika shule kwa jumla wanafaa kujukumika kufanikisha haya kwa ushirikiano.Matukio yalishuhudiwa katika Shule ya Upili ya Sigalame iliyoko kwenye Kaunti ya Busia ni kinyume cha matarajio haya.

Mojawapo ya mabweni ya shule hii iliripotiwa kuchomwa na wanafunzi kuagizwa kwenda nyumbani hadi uchunguzi kamili kuhusu tendo hilo la uhalifu huo ukamilike na suluhisho kamili na kudumu kupatikana.

Mbali na hasara kutokana na uharibifu wa vifaa vya wanafunzi katika bweni, hakuna madhara ya kiafya yalitoripotiwa kuwakumba wanafunzi.

Hali inayotamausha katika tukio hili ni kwamba, hii ni bweni la nne kuchomeka ndani ya mihula miwili pekee na bado kiini cha uhalifu huu hakijafichuliwa licha ya uchunguzi kufanywa kila wakati.

La wazi ni dai kwanza wanafunzi hawahusiki kabisa!Kulingana na Bodi ya Usimamizi (BOM) katika shule hii, tayari imewasilisha kwa Tume ya Kuajiri Walimu nchini (TSC) malalamiko na ushauri kuhusu jinsi ya kukabili tatizo hilo lakini hatua ya dharura ilivyokatikana haikuchukuliwa na TSC kwa wakati uliofaa.

Kuna malalamiko chungu nzima ya usimamizi mbaya na ufisadi katika utoaji tenda ambapo kidole cha lawama kinaelekezewa Mwalimu mkuu na naibu wake.

Ni aibu pia kuona Shule ya Upili ya Ofafa Jericho katika Kaunti ya Nairobi ikijipata katika orodha hii ya uchomaji bweni siku moja baada ya wenzao wa Sigalame.

Tume ya TSC ikishirikiana na wizara ya Elimu inafaa kuingilia kati masuala ya kinidhamu kama haya kabla hayajaenea nchini ili kuhakikisha shule zinasimamiwa na walimu wenye maadili ya kipekee.

You can share this post!

Mbunge atumai Gideon Moi atanyaka tiketi ya OKA

Watoto wa demu wadharau sponsa