• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 10:06 AM
AKILIMALI: Magurudumu yanamvunia hela, ni kutia bidii tu!

AKILIMALI: Magurudumu yanamvunia hela, ni kutia bidii tu!

Na WINNIE ONYANDO

BAADHI ya watu hutupa magurudumu baada ya matumizi ya muda ila kwake Joseph Mwaniki, 33, gurudumu lililotumika bado lina manufaa tele kwake.

Joseph alianza kazi hii ya kutumia magurudumu kuunda bidhaa tofauti mnamo 2012, alipoacha kazi kama ajenti wa kampuni moja ya bima.

“Mimi hukusanya magurudumu yaliyotumika, kuyasafisha na kutengeneza bidhaa tofauti. Pesa ninazopata kutoka kwayo ni nyingi hata mtu hawezi kuamini,” akaeleza Akilimali ilipozuru karakana yake katika soko la Kariokor, jijini Nairobi.

Yeye hutumia magurudumu hayo kutengeneza viatu, kanda, kamba za kufungia mizigo na pia zinazotumika katika uundaji wa makochi; sofa.

Hata hivyo, katika uundaji wa vitu tofauti, pia kuna vile ambapo hulazimika kujumuisha ngozi ya ng’ombe au ngamia, gundi na pia vitambaa pamoja na madoido mengine hasa kwa viatu ili kuvutia wateja.

Kwa siku, anasema, yeye hutengeneza zaidi ya jozi 50 za viatu na kujipatia faida ya takriban Sh5,000.

Kila jozi huwa anaiuza kwa kati ya Sh200 na Sh400.

“Mara nyingi mimi huuza viatu ninavyounda kwa wateja wa jumla, hasa kutoka jamii ya Wamaasai. Pia huwa ninawauzia wateja wa rejareja wanaofika kwa karakana yangu,” anaeleza.

Biashara hiyo anasema imemuwezesha kujiinua kimaisha kama kujenga nyumba nzuri na pia kumudu karo ya watoto wake wawili.

Hata hivyo, zipo changamoto na inayomkaba zaidi anasema ni ushindani mkubwa wa soko.

“Ubunifu ndio njia ya kujifaa katika biashara yoyote. Hii itakuwezesha kuwashinda washindani wako,” anashauri kuhusu mbinu anayotumia kuweza kukabiliana na changamoto hiyo.

You can share this post!

Samuel Eto’o kuwania urais wa Shirikisho la Soka la...

KAMAU: Mizozo UoN inatishia ndoto za vijana wetu