• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 5:46 PM
KINYUA BIN KING’ORI: Masharti ya wandani kisiki kwa ‘handisheki’ ya UhuRuto

KINYUA BIN KING’ORI: Masharti ya wandani kisiki kwa ‘handisheki’ ya UhuRuto

Na KINYUA BIN KINGORI

JUHUDI zilizoanzishwa na viongozi wa makanisa kupatanisha Rais Uhuru Kenyatta na naibu wake Dkt William Ruto, zinafaa kulenga maslahi ya Wakenya si binafsi ya viongozi hao wawili wenye mamlaka makuu serikalini.

Wandani wao wameanza kutoa masharti ambayo lazima yazingatiwe ili mapatano hayo kufanikiwa.

Aidha, wanalaumiana kwa kutoa vijisababu visivyo na maana, na huenda wakavuruga juhudi za viongozi hao kuridhiana.

Imebakia miezi 11 kwa serikali ya Jubilee kumaliza muda wake na kupisha utawala mpya baada ya uchaguzi mkuu 2022.

Lakini nyingi ya ahadi ambazo UhuRuto walitoa hazijatekelezwa.

Hakuna maendeleo ya kujivunia ambayo tumepata kipindi hiki cha pili, na katika kipindi hiki cha lala salama hatutarajii maendeleo yoyote ikiwa viongozi hao hawatazika tofauti zao.

Hivyo, kuna haja kubwa Wakenya kuunga mkono viongozi hao wapatane ili tuone ikiwa watasuka mipango ya haraka kuokoa wananchi na madhila ya uchumi mbaya sababu ya utendakazi duni wa serikali hii ya Jubilee.

Je, serikali ambayo viongozi wakuu wanatumia muda wao mwingi kulumbana, kuchimbana na kupigana kisiasa kwa manufaa yao, watarajia ipate muda lini kujua wananchi wamelemewa na ugumu wa maisha?

Je, wanaweza kupata suluhisho litakalohakikisha Wakenya wanaohangaika kwa makali ya njaa wamepata msaada wa chakula? Kushindwa kwa Jubilee kushughulikia matatizo yanayokumba Wakenya kumechochewa na uhasama kati ya Rais na Dkt Ruto.

Ajenda kuu ziliwekwa kando, miradi mingi kupuuzwa na mafaniikio waliyotuahidi ya maziwa na asali yamebakia kitendawili.

Badala yake, wamechochea chuki serikalini hadi bungeni ambako wabunge wanatekeleza wajibu wao kutegemea mrengo wao wa kisiasa wala si kwa manufaa ya wananchi walala hoi.

Leo hii tunaumizwa kwa bei ya juu ya mafuta baada ya wabunge kupitisha mswada wa kuongeza ushuru.

Maisha yataendelea kubakia magumu katika miezi michache inayokuja kabla uchaguzi, ikiwa Uhuruto hawatajitolea kumaliza uhasama wao.

Dkt Ruto ametangaza hadharani kwamba yuko tayari kufanya mazungumzo na Rais bila masharti, naye Rais anafaa kujtokeza kukumbatia maridhiano ili juhudi za viongozi wa makanisa zifaulu.

Pia watumie nafasi hiyo kuelezea Wakenya kiini cha uhasama wao maana hatujui kilichoenda mrama baada ya uchaguzi wa 2017.

Rais na Dkt Ruto waweke kando maslahi ya binafsi na matamanio ya kisiasa ya 2022 ili kulenga msamaha na masikizano bila unafiki.

Taifa linahitaji mshikamano wao ili kumaliza baa la njaa, kuimarisha udhibiti wa corona na utoaji chanjo yake, kuunda nafasi za ajira kwa vijana, kuboresha elimu kwa kutatua changamoto zinazotishia ubora wa mtaala wa CBC, kupunguza gharama ya maisha, na kukamilisha miradi ya maendeleo kabla Agosti 2022.

Rais Kenyatta atafaulu kuacha nchi iliyo salama na yenye amani na umoja iwapo atapatana na naibu wake ili wamalize safari yao pamoja.

You can share this post!

KAMAU: Mizozo UoN inatishia ndoto za vijana wetu

Mudavadi akejeli vigogo ‘kudandia’ sera zake