• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
TAHARIRI: Midahalo endelevu itachochea ustawi

TAHARIRI: Midahalo endelevu itachochea ustawi

KITENGO CHA UHARIRI

NYAKATI za kampeni za kisiasa husheheni matumizi tele ya propaganda za kisiasa ambapo washindani mbalimbali huzitumia kuwaumbua wenzao, hasa uchaguzi unapokaribia.

Ni mtindo ambao umekuwepo kwa muda mrefu tangu mwanzo wa tawala zilizojikita kwenye mfumo wa kidemokrasia katika maeneo kama Ugiriki na falme ya Roma.

Nchini Ugiriki, washindani wa nyadhifa mbalimbali za uongozi katika miji ya Athens na Sparta walitumia majarida maalum kuelelezea mikakati ambayo wangetumia kuboresha uongozi.

Kando na kujumuisha mikakati yao, walikosoana, japo kwa njia ambazo zilizua midahalo ya kuvutia miongoni mwa wenyeji wa miji hiyo miwili mikuu.

Mfumo huo ndio uliokua na kupanuka kabisa kiasi cha kuigwa na nchi kama Amerika na Uingereza.

Lengo kuu la tathmini hii ni kubuni msingi kuhusu chimbuko na athari za matumizi ya propaganda kwenye siasa.

Nchini Amerika, midahalo ambayo hufanyika miongoni mwa washindani wa urais huwa ni kuumbuana na kukosoana, ingawa huendeshwa kwa njia ya kuwazindua wafuasi wa kila upande.

Hapa Kenya, tumeona majaribio kadhaa ya maandalizi ya mdahalo wa kitaifa miongoni mwa wawaniaji wakuu wa urais.

Jaribio la kwanza lilikuwa mnamo 2013 huku zoezi la pili likiwa 2017.

Kwenye mdahalo uliofanyika 2013, Wakenya walipata nafasi ya kufuatilia kwa kina mipango ambayo wawaniaji husika walikuwa nayo ili kuiboresha nchi.

Jambo lilo hilo lilifanyika mnamo 2017, ingawa halikufaulu kama 2013 kutokana na migawanyiko ya kisiasa iliyokuwepo nchini, hasa kati ya mrengo wa Jubilee, ulioongozwa na Rais Uhuru Kenyatta na Nasa, ulioongozwa na Raila Odinga.

Tunapokaribia uchaguzi mkuu wa 2022, Baraza la Wahariri Kenya (KEG) limetangaza Julai 12 na 26 kuwa tarehe ambapo midahalo hiyo itafanyika. Hata hivyo, swali ni: Midahalo hiyo itafaulu kutokana na migawanyiko ya kisiasa iliyopo nchini?

Kosa kubwa ambalo vigogo wakuu wa kisiasa nchini wanafanya ni kuumbuana na kukosoana isivyofaa. Wengine hata wanatusiana hadharani kwa kisingizio cha kushindana.

Matumizi yafaayo ya propaganda hukitwa kwenye sera za mgombea husika wala si mwenendo wake, familia, marafiki au jamaa zake.

Nchini Amerika, wawaniaji hukosana kwa misingi ya sera na manifesto zao wala si sifa au familia zao.

Kosa hilo ndilo hujenga taharuki na migawanyiko ya kikabila isiyofaa.

Ni wakati wanasiasa wafahamu kuwa propaganda huwa njia ya kuzua midahalo endelevu wala si kutusiana.

You can share this post!

Anayedaiwa kujaribu kuua Kosewe ‘atikisa’ kesi

AS Roma ya kocha Jose Mourinho yapepeta Udinese na kuingia...