• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 4:36 PM
KAMAU: Ni aibu kuwatelekeza mashujaa waliopigania uhuru

KAMAU: Ni aibu kuwatelekeza mashujaa waliopigania uhuru

Na WANDERI KAMAU

KULINGANA na majarida mbalimbali ya historia, vita vya Maumau ni miongoni wa harakati zinazotambulika duniani kote kutokana na jinsi Wakenya walivyojitolea kuukabili utawala wa kikoloni wa Waingereza.

Wasomi wa historia wanasema kuwa kwa namna moja, kujitolea kwa Wakenya kwenye vita hivyo ndiko kulikowapa msukumo Waafrika wengine katika nchi kama Algeria, Msumbiji, Angola na Afrika kusini.

Nchini Algeria, vita vya ukombozi wa taifa hilo vilidumu kati ya mwaka 1954 hadi 1962, wakati taifa hilo lilijinyakulia uhuru wake kutoka kwa Ufaransa.

Vikosi vya Ufaransa vilijipata taabani, wakati raia wa Algeria walijitokeza kwa ujasiri kuwakabili kutokana na dhuluma ambazo walikuwa wakiwafanyia.

Nchini Msumbiji, vita vya ukombozi vilidumu kati ya 1964 hadi 1974, wakati taifa hilo lilipata uhuru wake kutoka kwa Ureno, kupitia kubuniwa kwa serikali ya umoja wa kitaifa.

Nchini Angola, harakati hizo zilidumu kati ya 1961 hadi 1974.Bila shaka, ni wazi kuwa vita vya Maumau vilibuni msingi mzuri wa harakati hizo, kwani vilidumu kati ya 1952 hadi 1958.

Licha ya vita hivyo kubuni msingi thabiti kuhusu jinsi Afrika ilipigania uhuru wake, inasikitisha kuwa hadi sasa, Kenya ni miongoni mwa nchi ambazo zimewatelekeza mashujaa hao.

Hadi sasa, wapiganaji wa Maumau wamekuwa wakilalamikia jinsi serikali nyingi zimekosa kushughulikia maslahi yao tangu miaka ya sitini.

Hii ni licha ya Uingereza kutoa mabilioni ya fedha kwa wapiganaji hao kulipwa kama ridhaa, kutokana na mateso na dhuluma ambazo walipataSerikali ya Mzee Jomo Kenyatta, marehemu Daniel Moi na Rais Mstaafu Mwai Kibaki zilifumbia macho vilio vyao vyote.

Hata hivyo, Bw Kibaki alijaribu jinsi awezavyo kushughulikia maslahi yao, ingawa juhudi hizo hazikuzaa matunda sana.

Ni wakati wa utawala wa Mzee Kibaki ambapo minara ya mashujaa kama Dedan Kimathi na mwahaharakati Tom Mboya ilijengwa, kama njia ya kukumbuka michango waliyotoa kwenye harakati za ukombozi wa nchi.

Inasikitisha kuwa wapiganiaji wengi wamekuwa wakidai kiwango kikubwa cha fedha walizopaswa kulipwa ziliporwa na maafisa na mawakili waliosimamia taratibu za kuwalipa.

Je, Kenya kwelininawajali wazalendo wake?

Imefika wakati tujifunze kutoka kwa nchi kama Afrika Kusini, kuhusu njia bora za kuwathamini mashujaa na wanaharakati waliopigania uhuru.

[email protected]

You can share this post!

MUTUA: Wakenya walio ng’ambo wana haki ya kupiga kura

Tope la Jubilee latesa Raila