• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 4:55 PM
JAMVI: Nyota ya kisiasa ya Karua inaingia doa?

JAMVI: Nyota ya kisiasa ya Karua inaingia doa?

Na WANDERI KAMAU

HATUA ya kutangazwa kwa kiongozi wa Narck-Kenya, Bi Martha Karua, kama kaimu msemaji wa ukanda wa Mlima Kenya, imeibua maswali kuhusu ikiwa ametia doa sifa yake kama kiongozi wa kitaifa.

Bi Karua alitwikwa jukumu hilo kwenye kikao maalum cha viongozi wa ukanda huo, kilichofanyika mwanzoni mwa wiki hii, mjini Naivasha, Kaunti ya Nakuru.

Waliokuwepo kwenye kikao hicho ni Bi Karua, aliyekuwa gavana wa Kiambu, William Kabogo na mbunge Moses Kuria (Gatundu Kusini).

Bw Kabogo ni kiongozi wa chama kipya cha Tujibebe Wakenya Party (TWP) huku Bw Kuria akiwa kiongozi wa Chama cha Kazi (CCK).

Viongozi hao walisema walifanya uamuzi huo baada ya kushauriana na viongozi wenzao kutoka sehemu mbalimbali katika ukanda huo.

Vile vile, walisema kuwa uamuzi wa kumtawaza Bi Karua kushikilia nafasi hiyo ulitokana na hali kuwa yeye haegemei mrengo wowote wa kisiasa.

Hata hivyo, wadadisi wa siasa wameeleza kuwa, ingawa huenda hatua hiyo inaonekana kumkweza Bi Karua kisiasa katika ukanda huo, kuna uwezekano ikampaka tope na kushusha nyota yake kitaifa kama mwanamageuzi anayeheshimika.

Kulingana na Prof Ngugi Njoroge, ambaye ni mchanganuzi wa siasa, kukwezwa kwa Bi Karua kama kaimu msemaji wa ukanda huo kutamwingiza kwenye “siasa chafu” za ushindani wa yule anayepaswa kuwa mrithi wa Rais Uhuru Kenyatta.

“Ni wazi kuwa kuna ushindani mkubwa ambao umejitokeza miongoni mwa wanasiasa wanaolenga kumrithi Rais Kenyatta. Ikizingatiwa Bi Karua amekuwa kwenye ligi ya kisiasa ya kitaifa, kuna uwezekano mkubwa akaanza kupigwa vita na wanasiasa wanapania kuchukua nafai hiyo,” akasema Prof Njoroge.

Bi Karua ni miongoni mwa viongozi wa eneo hilo ambao wamekuwa kwenye ulingo wa siasa kwa muda mrefu.

Alijitosa kwenye ulingo wa siasa katika miaka ya tisini, alipowania ubunge katika eneo la Gichugu, Kaunti ya Kirinyaga na kuibuka mshindi.

Alihudumu kama waziri wa Maji na Haki na Masuala ya Katiba katika serikali ya Rais Mstaafu Mwai Kibaki, hadi alipojiuzulu mnamo 2009.

Vile vile, alikuwa miongoni mwa viongozi walioshiriki katika Mazungumzo ya Serena baada ya ghasia za uchaguzi tata wa 2007, kumtetea Bw Kibaki.

Bi Karua alikuwa katika upande Bw Kibaki na chama cha PNU, akiwa pamoja na maseneta Moses Wetang’ula (Bungoma) na Prof Sam Ongeri (Kisii).

Kiongozi huyo pia aliwania urais mnamo 2013, ingawa hakuibuka mshindi.

Mnamo 2017, aliwania ugavana katika Kaunti ya Kirinyaga ingawa alishindwa na Gavana Anne Waiguru.

Wadadisi wanasema kuwa Bi Karua amejijengea sifa nzuri ya kiongozi anayeheshimika sana nchini na kimataifa, kwani kando na siasa, amekuwa akitumia taaluma yake ya uwakili kuwatetea wananchi.

“Hata ingawa Bi Karua analenga kurejea nyumbani kisiasa kama livyofanya mnamo 2017, nadhani kuna njia mbadala ambayo angetumia badala ya kukubali uteuzi wa kuwa msemaji wa Mlima Kenya. Kuna uwezekano mkubwa akajitosa kwenye vita na makabiliano ya kisiasa ambayo tumekuwa tukishuhudia baina ya mirengo mbalimbali katika ukanda huo,” asema Bw Ochieng’ Kanyadudi, ambaye ni mdadisi wa siasa.

Baada ya uteuzi wake, Bi Karua alijitenga na madai ya kuwa mwanachama wa mrengo wowote wa kisiasa, akishikilia nia yake ni kuhakikisha eneo hilo limeungana ili kuwa na sauti moja kwenye uchaguzi mkuu wa 2022.

“Mimi si mwanachana wa mrengo wowote. Ni mwanasiasa huru, anayelenga kuhakikisha watu wetu wamezungumza kwa sauti moja, kinyume na ilivyo sasa. Tunapaswa kuungana na kubuni njia tutakayofuata kwa wawaniaji wote wanaofika katika eneo letu kutuomba kuwaunga mkono,” akasema Bi Karua.

Mwanasiasa huyo amekuwa kiongozi wa Narc-Kenya kwa muda mrefu, akikitaja kuwa chama huru chenye misimamo yake kisiasa.

Kufikia sasa, viongozi waliotangaza ama kuonyesha nia ya kumrithi Rais Kenyatta ni aliyekuwa Waziri wa Kilimo, Mwangi Kiunjuri, magavana Mwangi wa Iria (Murang’a), Francis Kimemia (Nyandarua), Waiguru (Kirinyaga) kati ya wengine.

Hata hivyo, nia zao zimeandamwa na migawanyiko mikali, ambapo kwa sasa, kuna mirengo ya kisiasa ya ‘Kieleweke’ na ‘Tangatanga.’

Mrengo wa ‘Kieleweke’ umekuwa ukimtetea Rais Kenyatta huku ‘Tangatanga’ wakimtetea Naibu Rais William Ruto, kwenye nia yake kuwania urais 2022.

Bw Kanyadudi anasema kuwa kukubali nafasi hiyo, huenda Bi Karua analenga kuimarisha nafasi yake kuwania ugavana Kirinyaga, ikizingatiwa anakabiliwa na ushindani mkubwa kutoka kwa Mwakilishi wa Wanawake Wangui Ngirichi.

“Ilivyo sasa, Bi Karua ana kibarua kigumu kuwakabili Bi Ngirichi na Gavana Waiguru, ambao washatangaza azma ya kuwania ugavana. Kwa upande mmoja, nafasi hiyo itamsaidia kuinua nyota yake kisiasa, ila ajajipata tope ikiwa hatajiepusha na mizozo ya urithi ambayo huenda ikaibuka,” akasema mdadisi huyo.

You can share this post!

Real Madrid na Villarreal ni nguvu sawa La Liga

Bruno Fernandes asema hataachia Ronaldo jukumu la kuchanja...