• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 10:08 PM
PATA USHAURI WA DKT FLO: Kwa nini mjamzito huvuja damu puani?

PATA USHAURI WA DKT FLO: Kwa nini mjamzito huvuja damu puani?

Mpendwa Daktari,

Ni nini kinachosababisha kuvuja damu kutoka puani na kwenye ufizi ukiwa mjamzito?

Christine, Nairobi

Mpendwa Christine,

Wanawake wengi hukumbwa na shida ya kutokwa na damu puani wakati wa ujauzito na mara nyingi hali hii ni kawaida.

Lakini baadhi ya wanawake hukumbwa na wasiwasi wasijue la kufanya.

Sababu zinazochochea hali hii hutegemea na mtu binafsi.

Wanawake wajawazito kwa kawaida huwa na asilimia 30 hadi 50 zaidi ya mzunguko wa damu mwilini ikilinganishwa na watu wa kawaida.

Hii huhitajika ili kudumisha afya ya mtoto tumboni.

Baadhi ya masuala yanayochochea hali hii wakati huu ni kupanuka kwa mishipa ya kupitisha damu kwani damu inayosukumwa huongezeka wakati wa ujauzito.

Aidha kuna mafua yanayosababisha utandio kuwa mkavu na hivyo kusababisha mwasho.

Pia kuna ongezeko la homoni za estrogen na progesterone wakati wa ujauzito ambazo huongeza mzunguko wa damu mwilini.

Ongezeko hili husababisha damu kuvuja kutoka puani.

Mbali na hayo, hali hii yaweza sababishwa na kuchanua pua kwa nguvu, kwani hii husababisha mwasho na hata kutokwa na damu.

Wanawake wajawazito kwa wingi hushuhudia kufungamana kwa pua.

Ili kukabiliana na hali hii, tumia mbinu mbalimbali ili kudumisha unyevu chumbani hasa unapolala.

Pia, usichanue pua kwa nguvu hasa ukiwa na mafua. Tumia karatasi ya shashi yenye unyevu.

Kunywa maji au viowevu kwa wingi wakati wa mchana ili kunyoosha utando puani.

Aidha, tumia dawa maalum inayonyunyizwa kwenye pua au mafuta ya kujipaka ya petroli ikiwa unakumbwa na hali hii kwa wingi.

Hii itazuia kukauka kwa utando puani.

Pia usichokore pua na acha mdomo wazi unapopiga chafya ili kupunguza msukumo puani.

Pia ongeza kiwango cha virutubisho vya vitamini C kwenye mlo kwani huharakisha kupona kwa seli iwapo kuna majeraha.

Mpendwa Daktari,

Mwanangu wa kiume mwenye miaka miwili amekuwa akivuja mkojo kwa mwezi mmoja sasa.

Nimejaribu aina tofauti za dawa kutoka dukani lakini tatizo halitoweki.

Napaswa kufanya nini?

Jennifer, Mombasa

Mpendwa Jennifer,

Katika umri wa miaka miwili, watoto wengi hawajajua kwenda choo vilivyo na hata kwa wale wanaojua, ni kawaida kushindwa kujidhibiti mara kwa mara.

Masuala mengine ambayo yanaweza chochea tatizo hili ni pamoja na wasiwasi; mabadiliko ya kimazingira au matatizo ya kifamilia; dhuluma (matusi, kimwili, kimapenzi au kutelekezwa); tumbo kuvimba; kisukari; maambukizi kwenye mfumo wa mkojo; matumizi ya kafeini; usingizi wa pono au ikiwa ana matatizo ya kibofu.

Mpeleke mwanao akaguliwe na daktari kuthibitisha hali yake ya kiafya. Kuna dawa ambayo hupewa watoto wenye umri mkubwa (wa zaidi ya miaka sita).

Kumbuka kwamba dawa hii haipaswi kupewa mtoto wa miaka miwili, na unashauriwa kuipata kutoka hospitalini baada ya kufanyiwa uchunguzi wa kutosha.

You can share this post!

Watford waajiri kocha Claudio Ranieri kujaza pengo la Xisco...

TAHARIRI: Vijana wapewe vitambulisho upesi