• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 4:25 PM
Wakewenza wakazia buda asali

Wakewenza wakazia buda asali

Na TOBBIE WEKESA

LWANDA

JOMBI mkazi wa hapa alijipata pabaya baada ya wake zake kuamua kumnyima asali.

Inasemekana wakewenza walikubaliana kumnyima jamaa mizinga yao hadi ile siku atakapowalipia mahari.

Kulingana na mdokezi, wakewenza hao waliudhika sana na namna jamaa alivyokuwa akiendesha maisha yake bila kujali.

Duru zinasema jombi alipenda maisha ya starehe na kula vitu vizurivizuri.

Inadaiwa baada ya kuishi na mume wao kwa miaka mingi bila kuonyesha dalili zozote za kupeleka mahari kwa yeyote kati yao, waliamua kwa kauli moja kumkausha chumbani.

Habari zilizotufikia zinasema polo alipogundua kwamba mambo si shwari, aliamua kuwaonya wake zake huku akitishia kuwatimua wote.

“Naona mmeanza tabia ambayo sijui mlitoa wapi. Kama ni kuwalisha mimi nawalisha sawasawa. Mmesikilizana kuninyima haki yangu ya ndoa,” jamaa aliwazomea.

Inasemekana maneno yake yalikuwa ni kama raia kurusha jiwe ndani ya kituo cha polisi.

“Huna aibu hata kidogo. Wanaume wenzako wameshalipia mahari wake zake. Wewe unasubiri nini. Ama unataka Yesu arudi akukumbushe kupeleka mahari kwetu,” polo alifokewa.

Majirani walibaki kutazama sinema bila kuingilia kati.

“Tumeamua ya kwamba sisi kama wake zako hutakuwa ukitukaribia. Utakuwa ukila kwa macho,” wakewenza waliapa.

Kwa kuhofia kuaibishwa, jamaa aliamua kuondoka kimyakimya.

“Acha tukuambie ukweli. Bendera zetu hatutawahi kukuteremshia tena. Ulikuwa umezoea kuziteremsha wakati wowote utakapo,” mke wa pili alifoka.

Inadaiwa jamaa alitamani ardhi ipasuke immeze mzimamzima.

“Wewe mtu sampuli gani. Chumbani unataka madikomadiko lakini hutaki kutoa mahari. Utajipanga kuanzia leo. Tumejanjaruka,” mke wa kwanza aliongeza.

  • Tags

You can share this post!

Kocha wa Kenya Morans Liz Mills atuzwa mpira wa dhahabu kwa...

Seneta wa zamani awasilisha kesi uchaguzi mkuu 2022...