Na RICHARD MUNGUTI
ALIYEKUWA waziri wa michezo Rashid Echesa aliyeshtakiwa kwa sakata ya Sh39bilioni aliachiliwa huru Ijumaa baada ya mahakama kusema hakukuwa na ushahidi wa kutosha.
Echesa aliachiliwa na hakimu mwandamizi Kenneth Cheruiyot aliyetoa uamuzi saa moja unusu jioni. Lakini hakimu huyo alimpata na kesi ya kujibu mfanyabiashara Chrispin Oduor Odipo. Odipo alipatikana akiwa na stampu kutoka idara ya jeshi (DoD) bila idhini.
Akitoa uamuzi Cheruiyot alisema upande wa mashtaka haukuwasilisha ushahidi jinsi waziri huyo alihusika katika kughushi kandarasi. Echesa na washtakiwa wenzake walikabiliwa na mashtaka ya kupokea zaidi ya Sh11.5milioni kutoka kwa wafanya biashara wawili wa kimataifa Kozlowski Stanley Bruno na Mamdough Mostafa Lofty kwa madai watawasaidia kupata kandarasi ya kuuzia idara ya kijeshi silaha.
Bruno ni raia wa Amerika na kinara wa kampuni ijulikanayo ECO Advanced Technologies ilhali Mostafa ni raia wa Misri. Upande wa mashtaka uliwaita mashahidi 18.