NA BRIAN OCHARO
MAAFISA wa polisi wamedai kuwa, washukiwa wawili waliohusishwa na wizi wa Sh700, 000 za mwajiri wao walizipeleka kwa mganga ili ziongezeke.
Kwenye hati zilizowasilishwa katika Mahakama ya Mombasa, polisi wamedai washukiwa Zanjabil Musumba Mbururu na Desmol Dust Wamalwa, waliagizwa na mganga kuziweka kwenye chungu bila kukifungua kwa miezi mitatu ili ziongezeke.
Inadaiwa mganga aliwaonya kama wangekaidi ushauri wake, pesa hizo zingegeuka jivu.
Walikana mashtaka mbele ya Hakimu Mkuu Mkazi David Odhiambo, wakaachiliwa kwa dhamana ya Sh300, 000 pesa taslimu kila mmoja.
Imedaiwa walipanga njama na wenzao kumwibia Bw Kumar Prateshkumar Prassana, mnamo Mei 10 na 13, 2023 mtawalia eneo la Changamwe.
Inasemekana Bw Mbururu ndiye alipewa pesa kuzishikilia lakini akatoweka nazo.
Alikamatwa Mombasa huku Bw Wamalwa akikamatwa Mumias, Kaunti ya Kakamega.
Imedaiwa Bw Wamalwa alipohojiwa, alidai alikuwa amempa mzazi wake pesa hizo.