• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 9:55 AM
Jaji ajiondoa kusikiliza kesi ya ufisadi

Jaji ajiondoa kusikiliza kesi ya ufisadi

Na RICHARD MUNGUTI

JAJI David Majanja amejiondoa katika kesi ambapo msajili mkuu wa Idara ya Mahakama Bi Anne Amadi ameshtakiwa kwa ulaghai wa Sh89 milioni katika kashfa ya dhahabu.

Bi Amadi alishtakiwa na raia wa Uingereza Bw Demetrios Bradshaw akidai msajili huyo alimtapeli akidai atampelekea kutoka Kenya hadi Dubai.

Akijitoa katika kesi hiyo Jaji Majanja alisema yeye na Bi Amadi ni wanachama wa tume ya idara ya mahakama (JSC) na “hawezi kusikiza kesi hiyo ya ufisadi dhidi ya msajili huyo.”

Jaji huyo alisema Bi Amadi ndiye msajili mkuu wa mahakama zote nchini na kesi yake yapasa kusikizwa na jaji mwingine.

Jaj Majanja aliagiza kesi hiyo iwasilishwe mbele ya Jaji Alfred Mabeya anayesimamia kitengo cha kesi za biashara katika mahakama kuu.

Alisema Jaji Majanja aking’atuka: “Mimi ni mwanachama wa JSC ambapo Bi Amadi ni katibu mkuu wa JSC. Siwezi endelea kusikiza kesi hii.”

Na wakati huo huo, Bi Amadi aliwasilisha ushahidi katika mahakama kuu akisema “hakuhusika na sakata hiyo.”

Msajili huyo alisema ijapokuwa kampuni ya mawakili ya Amadi & Associates Advocates ni yake alijiuzulu alipoajiriwa katika idara ya mahakama.

“Mwanangu ndiye anayesimamia kampuni yangu ya mawakili ya Amadi & Associates Advocates. Nilikuwa mwanzilishi wa kampuni hii ya mawakili lakini nilijiuzulu nilipopata kazi katika idara ya mahakama,”alisema Bi Amadi.

Jaji Majanga aliagiza kesi hiyo itajwe mbele ya Jaji Mabeya Mei 31, 2023 kwa maagizo zaidi.

Jaji Majanja alikataa ombi la mawakili James Ochieng na Samson Nyaberi akaunti za Bi Amadi na za kampuni ya mawakili ya Amadi & Associates zifunguliwe.

 

  • Tags

You can share this post!

Rais wa Tanzania ajitokeza kusaidia Yanga kwa hali na mali

ZARAA: Nyasi maalum inayopatia wafugaji matumaini tele

T L