NA ANGELINE OCHIENG
MWENYEKITI mpya wa Baraza la Wazee wa jamii ya Waluo ‘Ker’ atajulikama baada ya Juni 10, 2023, kiongozi wa Azimio La Umoja-One Kenya Raila Odinga ametangaza.
Raila ambaye ni mlezi wa baraza hilo amesema hayo Alhamisi baada ya kuhudhuria mkutano wa kwanza wa baraza hilo ulioandaliwa jijini Kisumu.
“Wanachama wote kutoka kaunti ndogo zote zilizoko katika eneo pana la Luo Nyanza watahusishwa kuamua ni nani atakuwa ‘Ker’ mpya,” amesema Raila.
Mwenyekiti mpya atarithi nafasi hiyo iliyoachwa wazi baada ya kifo cha Ker Willis Opiyo Otondi kilichotangazwa mnamo Ijumaa, Februari 17, 2023.
Ifahamike kwamba hilo litatokea tu baada ya wazee kufanya matambiko ya mwisho kwenye kaburi la marehemu Otondi aliyeenziwa sana. Matambiko yatafanyika mwezi ujao wa Juni.
Otondi alikuwa babu yake mwanahabari Willis Raburu wa kituo cha televisheni cha Citizen.