NA RICHARD MAOSI
Kinara wa Azimio Raila Odinga?raila amechamba serikali kwa kuwauzia raia mbolea, ambazo zimetolewa kama msaada na serikali ya Urusi.
Katika mkutano wa hadhara alipokuwa akiwahutubia wananchi katika Kaunti ya Kisii, Raila alisema mambo ya Kilimo yako chini ya Serikali ya Ugatuzi wala sio serikali kuu.
Raila ameomba serikali kutoa pesa kwa serikali za Kaunti ili zisaidie kwenye usambazaji wa mbolea, badala ya kujilimbikizia majukumu ya Kaunti.
“Serikali isiseme itanunua mbolea na kukabidhi Kaunti zisambaze kwa wakulima kwa sababu hiyo sio kazi yao,”akasema.
Aidha Odinga ametupilia mbali madai ya kupunguza bei ya mbolea kutoka Sh6000 hadi Sh2500, akidai hiyo mbolea imetolewa bure na serikali ya Urusi igawanywe kwa wakulima bure.
Amesisitiza kuwa majukumu ya serikali za Kaunti yasiingiliwe na Serikali kuu.
Anasema serikali walipatiwa tani 34,000 wakaongeza mchanga na kufikisha tani 100,000 ili watu binafsi wajitengenezee faida nono.
Hili linajiri siku chache baadhi ya wakulima wakidai hawajapata mbolea ya bei nafuu ingawa serikali imesisitiza kusambaza mbolea hizi kwenye mashirika ya Kitaifa ya kuhifadhi Mazao na Nafaka NCPB.