• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 7:55 AM
Wito EACC ichunguze maafisa wa elimu

Wito EACC ichunguze maafisa wa elimu

Na MAUREEN ONGALA

CHAMA cha Walimu wa Sekondari (KUPPET) kimeomba Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi (EACC) ianzishe uchunguzi dhidi ya maafisa wawili wa elimu Kaunti ya Kilifi.

Walimu hao wanataka uchunguzi uanzishwe dhidi ya mkurugenzi wa elimu anayeondoka, Bi Eunice Khaemba na aifsa wa kutathmini ubora wa elimu, Bw Isaac Wasai wakiwahusisha na sakata za ufisadi.

Akizungumza katika kikao cha wanahabari afisini mwao mjini Kilifi, mwenyekiti wa KUPPET tawi la kaunti hiyo, Bw Caleb Mogere alidai kuwa wawili hao walihusika katika njama za kuhangaisha baadhi ya shule zilizotaka kusajiliwa, na pia kutatiza juhudi za bodi za usimamizi wa shule nyingine kuboresha miundomsingi.

“Kuna miradi mingi katika shule mbalimbali ambayo imekwama kwa sababu wamekataa kuidhinisha na tunashuku kuna ufisadi katika suala hilo zima,” akasema.

Malalamishi yao yanahusu pia kukwama kwa juhudi za kugeuza shule za kutwa ziwe za mabweni ili kuongeza idadi ya wanafunzi wanaopokea elimu.

Hata hivyo, Bi Khaemba alikanusha madai hayo akasema masuala yanayotajwa hayatekelezwi na afisi yake kibinafsi wala afisa wa ubora wa elimu.

“Sina habari kuhusu shule zozote ambazo zimenyimwa usajili baada ya kutimiza mahitaji yanayotakikana. Ni muhimu itambulike kuwa usajili hufanywa na bodi wala si mtu binafsi,” akasema.

You can share this post!

Simulizi ya mama yashtua mahakama

Ruto akausha mahasla