NA WACHIRA MWANGI
WANAUME wawili wameaga dunia kutokana na majeraha waliyopata huku mmoja akipigania maisha yake baada ya maporomoko ya ardhi kutokea karibu na kivuko cha Likoni, kwenye Kisiwa cha Mombasa leo Alhamisi asubuhi.
Watatu hao walikuwa wamelala katika mojawapo ya mapango yaliyo kando ya eneo la Mama Ngina Waterfront wakati udongo uliporomoka na kuwaua wawili wao mwendo wa saa kumi na mbili asubuhi.
Mmoja alijeruhiwa, akaokolewa na kupelekwa katika Hospitali Kuu ya Mafunzo na Rufaa ya Pwani (CGTRH) kwa matibabu.
Inaaminika kuwa udongo ulilegea kufuatia mvua kubwa iliyonyesha katika siku chache zilizopita.
Kwa mujibu wa Bw Abdullahi Athman Kombo, ndugu wa mmoja wa marehemu, alikuwa amefika tu kumwamsha kaka yake wakati tukio hilo lilipotokea.
“Marehemu kaka yangu, Abdullah Mwaboza amekwenda. Nilikuwa naja kumwamsha ili twende kutafuta riziki lakini haikupangwa hivyo. Tumekuwa hapa tangu mwaka wa 2013 na ni mara ya kwanza tunakumbana na hali hii. Alikuwa pamoja na marafiki zake na inasikitisha,” Bw Kombo amesema.
Miili hiyo imepelekwa katika hifadhi ya maiti ya CGTRH.