Na SAMMY KIMATU
MAMIA ya waathiriwa wa moto na upepo mkali uliotokea katika mtaa wa mabanda wa Mukuru-Hazina, South B, kaunti ndogo ya Starehe wangali wanahangaika, majirani wakiwasaidia kwa kuwapa malazi.
Wengine wanaowasaidia waathiriwa ni marafiki, jamaa wao na wasamaria wema.
Uchunguzi wa Taifa Leo mnamo Jumatatu ulibaini kwamba wamiliki wa nyumba 80 zilizoteketea hawakuwa wamezijenga upya.
Waliozungumza na Taifa Leo walidaia uchumi ni mbaya wakipata changamoto ya kununua simiti, mbao na mabati wakisema bei yake ni ghali mno.
Bw George Otieno,60, fundi wa vifaa vya kielekroniki katika mtaa jirani wa Mukuru-Kayaba alisema alikuwa amemiliki nyumba nne hapo za kukodisha.
“Nimebaki bila kitu na sijui nitapata wapi pesa za kununua mabati na simiti wakati huu ambapo gharama ya maisha iko juu,” akasema.
Mwathiriwa mwingine, ambaye ni fundi wa kushona Bw Nicholas Koyo,48, alisema cherehani nne ziliteketea pamoja na nguo za wateja.
Aliongeza kwamba hakuna viongozi wa kisiasa waliotoa chochote cha msaada na kuongeza kwamba wanatarajia Mungu kuwafanyia muujiza kupata wafadhili ndiposa waanze maisha upya.
Mkuu wa polisi katika eneo la Makadara Bi Judith Nyongesa alisema polisi wanachunguza kisa hicho kubaini kilichosababisha moto huo.