NA JESSE CHENGE
IDARA ya polisi katika kaunti ya Bungoma imeweka mikakati kurejesha usalama eneo la Chepkitale, Mlima Elgon.
Kamanda wa polisi wa kaunti hiyo, Francis Kooli amesema kuwa uamuzi huo umetokana na ongezeko la visa vya utovu wa usalama eneo hilo.
Hali ya ukosefu wa usalama imesababisha wenyeji wa Chepkitale kutoa wito kwa Kooli kuwawekea kituo cha polisi.
Kwa upande wake Kooli, ameahidi kutuma maafisa wa polisi kudumisha usalama iwapo watapewa sehemu ya kulala.
“Tuko tayari kutuma maafisa katika eneo la Chepkitale lakini wanahitaji mahali pa kuishi. Tunaomba viongozi kuwatafutia sehemu ambayo wataishi. Tutashirikiana na jamii ili kuimarisha usalama,” akasema afisa huyo.
Kamanda Kooli aidha ameonya wanaoendeleza uhalifu, chuma chao ki motoni.
Kulingana na Kooli, imekuwa vigumu kwa askari kukabiliana na uhalifu kwa sababu wengi hutorokea nchi jirani ya Uganda punde wanapotekeleza uhalifu.
Ameahidi kutuma maafisa 20 katika eneo hilo kwa muda mfupi ili kushughulikia dharura iliyoko.
Hata hivyo, amewataka wahalifu kusalimisha silaha haramu wanazomiliki kwa polisi kabla ya kuchukuliwa hatua kali kisheria.