• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 10:08 PM
Kiongozi wa zamani wa Mungiki mafichoni akisakwa na DCI

Kiongozi wa zamani wa Mungiki mafichoni akisakwa na DCI

Na WANGU KANURI

MAAFISA wa upelelezi wa jinai (DCI) Nakuru wanamtafuta aliyekuwa kiongozi wa kundi haramu la mungiki, Maina Njenga, baada ya silaha mbili na kiasi kikubwa cha dawa za kulevya kupatikana nyumba inayodaiwa kuwa yake.

Maafisa hao pia waliwakamata watu nane wenye umri wa kati ya miaka 37 na 54 wakati wa msako huo katika kitongoji cha Ngomongo, wadi ya Dundori.

Mkuu wa DCI Mohammed Amin kwenye taarifa yake alisema kuwa moja ya silaha zilizopatikana ni bastola iliyotengenezwa nyumbani ambayo inaweza kufyatua, huku nyingine ikiwa ni bastola ya Tokarev ambayo nambari yake ya usajili imeharibiwa kwa makusudi.

“Vifurushi vitatu vya risasi tupu za milimita 9 pia vilipatikana vimefichwa katika moja ya vyumba ndani ya nyumba hiyo,” akaongezea.

Isitoshe, Bw Amin alisisitiza umuhimu wa ushirikiano wa umma na kuwahimiza wale wote wenye taarifa kuhusu aliko kiongozi huyo wa zamani wa Mungiki kuwasiliana na maafisa wa DCI.

Tukio hili linafuatia madai ya hivi karibuni ya Njenga mwenyewe akisema kuwa mnamo Mei 12, 2023 nyumba zake huko Nairobi, Nakuru, na Laikipia zilivamiwa na polisi.

Njenga, alielezea imani yake kwamba hatua hizi zilikuwa ni jaribio la kumzuia kuhudhuria mazishi ya Mukami Kimathi, mjane wa mpiganaji wa uhuru Dedan Kimathi.

Akilalamikia misako hiyo ya nyumba zake, Njenga alisema kuwa alikuwa akinyanyaswa kisiasa.

“Walisema wananihitaji. Sijui kwa nini, lakini mimi nafikiria hii ni siasa na unyanyasaji ambao unapaswa kukomeshwa,” akasema kupitia mahojiano ya awali.

Ni muhimu kutambua kwamba Njenga amekamatwa na kushtakiwa mara kadhaa hapo awali wakati mamlaka zilijaribu kumhusisha na kundi haramu la Mungiki.

Huku uchunguzi ukiendelea, umma unangoja taarifa zaidi kuhusu kesi hii ya kusisimua, ambayo tena imevuta umakini Njenga na tuhuma zake za kushiriki katika uhalifu.

  • Tags

You can share this post!

Sarakasi za Akothee Ufaransa akizuiwa kutumia majanichai ya...

Akothee: Msiniulize kuhusu wadhifa wangu wa Rais wa...

T L