NA RICHARD MUNGUTI
MAHAKAMA ya Rufaa Ijumaa imetupa kesi ya Bw Dennis Itumbi aliyeomba korti itoe maagizo ya kuruhusu Mawaziri Wasaidizi (CASs) 50 kuanza kazi.
Itumbi ambaye ni bloga anayeegemea mrengo tawala wa Kenya Kwanza, ni miongoni mwa walioteuliwa na Rais William Ruto.
Aliteuliwa kuwa CAS katika Wizara ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (ICT) na Uchumi wa Kidijitaji.
CASs waliapishwa rasmi mnamo Machi 23, 2023 lakini hawajaanza kazi kwa sababu Mahakama Kuu kwenye maagizo yaliyosomwa na Jaji Hedwig Ong’udi mnamo Ijumaa, Machi 24, 2023 iliwazima kutwaa rasmi majukumu yao hadi kesi inayopinga kuteuliwa kwao itakaposikilizwa na kuamuliwa.
Aidha mahakama iliwazima kupokea mishahara, kupokea marupurupu au mafao mengine hadi kesi iliyowasilishwa na Chama cha Wanasheria Nchini (LSK) na Katiba Institute itakaposikilizwa na kuamuliwa.