Na RICHARD MUNGUTI
MAHAKAMA Kuu imeamuru mali ya Sh537 milioni ya afisa katika Kaunti ya Nairobi itwaliwe.
Akiamuru mali ya Michael Auka Ajwang, Jaji Esther Maina alisema mfanyakazi huyo ambaye mshahara wake ni Sh21, 000 alishindwa kueleza jinsi alivyoipata.
“Auka alishindwa kueleza jinsi alivyopata mali yake ya Sh537 milioni ilhali mshahara wake ni Sh21,000. Shauku kwamba amejihusisha na ufisadi ni za kweli,” alisema Jaji Maina.
Jaji huyo alisema Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi Nchini (EACC) ilithibitisha kwamba ina ushahidi wa kutosha kumchunguza Auka.
“Mahakama hii imefikia uamuzi kwamba ombi la EACC kutwaa mali ya Auko una mashiko kisheria,” Jaji Maina alisema.
Miongoni mwa mali iliyotwaliwa na EACC ya Auka ni pamoja na magari ya kifahari 11, vipande tisa vya ardhi na hoteli ya kifahari iliyoko mjini Kisumu.
Mahakama ilielezwa kuwa hoteli hiyo inamilikiwa na kampuni ya Auka kwa jina Hydeout Riviera Limited.
Jaji huyo alisema mali hiyo inaaminika ilipatikana kwa njia isiyo ya haki.
EACC ilieleza mahakama kwamba inaamini Auka anajihusisha na ufisadi anapoendelea kuhudumia Kaunti ya Nairobi.