Na RICHARD MUNGUTI
MENEJA Mkurugenzi wa Shirika la Ukadiriaji wa Ubora wa Bidhaa Nchini (Kebs) Bernard Njiru Njraini na maafisa wakuu wa mamlaka ya Ushuru Nchini (KRA) wameshtakiwa kwa wizi wa sukari iliyokuwa imepigwa marufuku.
Sukari hiyo ni ya thamani ya Sh20 milioni.
Bw Njiraini alishtakiwa mbele ya Hakimu Mkuu Lucas Onyina pamoja na wakuu wa KRA Joseph Kiago Kaguru, Derrick Njeru Kago na Peter Njoroge Mwangi.
Wengine walioshtakiwa ni pamoja na mfanyabiashara Crispus Waithaka Macharia, aliyekamatwa punde tu alipotua katika uwanja wa ndege wa JKIA akitoka Dubai.
Wafanyabiashara wawili wa Mombasa, Mohammed Hassan Ali na Abdi Hirsi Yusuf almaarufu Blackie pia walishtakiwa kwa kashfa hiyo.
Bi Pollyanne Njeri Kamau alikana shtaka la kuiba sukari hiyo katika bohari la Thika.
Washtakiwa vilevile walikana kuiba magunia 20, 064 ya kilo 50 kila moja.
Sukari hiyo ilikuwa imeagizwa iharibiwe na KRA.
Kila mmoja aliachiliwa kwa dhamana ya Sh400, 000 baada ya kukanusha mashtaka.