NA LAWRENCE ONGARO
MSHTAKIWA wa kampuni ya mashamba ya Lesedi Properties mjini Thika, Geoffrey Kiragu, ambaye anakabiliwa na kesi ya ulaghai wa Sh5.47 milioni, amenyimwa dhamana na mahakama ya Thika.
Mshtakiwa alifikishwa mbele ya hakimu mkuu wa Thika Bi Stella Atambo ambaye aliyeagiza arudishwe rumande ya kituo cha polisi cha Muthaiga jijini Nairobi huku ripoti ya afisa wa probesheni ikitarajiwa baada ya wiki moja.
Alikabiliwa na mashtaka 12 ya kulaghai watu jumla ya Sh5.47 milioni kwa kuwauzia mashamba akitumia jina la Lesedi Developers.
Mnamo Jumatatu, Septemba 25, 2023, Kiragu alifikishwa mahakamani na akaomba apewe dhamana.
Aliwakilishwa na wakili mkongwe na mwenye tajriba Bw John Khaminwa akisaidiana na Daniel Gachau, Wilfred Nyamu, na Wanjiku Mwendwa.
Mnamo Septemba 21, 2023, hakimu Oscar Wabyaga alikuwa ameagiza ofisi ya probesheni iwasilishe ripoti yake ili mahakama iweze kupata mwelekeo wa kutoa dhamana.
Lakini jambo la kushangaza wakati afisa wa probesheni Bw Joshua Kirima, alipofika mahakamani alisema ya kwamba hakuwa ametayarisha ripoti kamili na kwa hivyo alitaka apewe muda wa wiki mbili ili kuwasilisha ripoti yake.
Maelezo hayo yaliwachanganya mawakili hao walioteta ya kwamba kucheleweshwa kwa ripoti hiyo kulisababisha mteja wao kuteseka akiendelea kuozea kwenye rumande kwa muda mrefu.
Kulingana na hakimu mkuu Bi Atambo, ripoti hiyo itawasilishwa mahakamani mnamo Oktoba 2, 2023, wakati hukumu kuhusu dhamana itatolewa.
Mshtakiwa, inadaiwa alitekeleza ulaghai wake kati ya Februari 5 na Machi 1, 2022, ambapo aliwapa watu matumaini ya kumiliki mashamba lakini baadaye wakagundua walikuwa wamelaghaiwa.