NA CECIL ODONGO
WITO wa umoja miongoni mwa waumini wa dini zote ili kukabili changamoto za nchi ulitawala Siku ya Hamasisho Kuhusu Uislamu katika msikiti wa Jamia jijini Nairobi, mnamo Jumamosi.
Wakati wa hafla hiyo, uongozi wa msikiti huo umewakaribisha Wakenya wa dini zote kutembelea msikiti, kufahamu mengi kuhusu Uislamu kwa kuuliza maswali kisha kupata majibu kutoka kwa wasomi wa dini hiyo.
Kwa mujibu wa Imam wa Jamia Sheikh Jamaldin Osman wamefungua milango ya msikiti ili kuleta uelewano na kuwezesha wengi kufahamu dini hiyo.
Sheikh Osman ametaja ubaguzi, fitina na ukabila akisema ni kati ya mambo ambayo yatatokomezwa iwapo kila dini itafungua milango kwa wale ambao si waumini wake kufahamu yaliyomo.
“Sisi hatulazimishi mtu kuingia Kusilimu lakini binadamu ana hiari kuingia Uislamu. Mimi nina jukumu la kufundisha ukweli kuhusu dini hii badala ya dhana zinazoenzwa si kweli. Wakristo na Waislamu wote wapo katika nchi kwa hivyo heshima na maelewano inapatikana tukitangamana na kufahamiana,” akasema Sheikh Osman.
Kwa mujibu wa Mkuu wa Daawa (Da’wah) Mohamed Sheikh amesema zaidi ya Wakenya 700 wamejitokeza katika msikiti huo ili kupata mafunzo na kujua mengi kuhusu Uislamu.