NA CHARLES WASONGA
RAIS William Ruto ametangaza kuwa serikali imejitolea kutimiza ahadi yake ya kuweka mawimbi ya mawasiliano ya WI-FI ya bure katika jumla ya vituo 25,000 kote nchini.
Akiongea mjini Embu mnamo Ijumaa, Rais Ruto alisema kuwa mpango huo utawasaidia wafanyabiashara wadogo kuendeleza biashara za mitandaoni kupitia mfumo ujulikanao kwa kimombo kama, ‘e-commerce’.
“Wale ambao watanufaika zaidi katika mpango huu wa mtandao wa mawasiliano bila kulipiwa ni mamilioni ya vijana hawa wetu ambao huendesha shughuli nyingi mitandaoni,” Rais akasema alipofungua rasmi maonyesho ya biashara ndogondogo, vyama vya ushirika, biashara na ukusanyaji ushuru katika uwanja wa Chuo Kikuu cha Embu.
Dkt Ruto pia alitumia nafasi hiyo kuzindua kituo cha Wi-Fi ya bure kutumiwa na wanafunzi, wahadhiri na wafanyakazi katika chuo hicho.
Kiongozi wa taifa aliandamana na Naibu wake Rigathi Gachagua, mawaziri Eliud Owalo (ICT), Moses Kuria (Biashara), Simon Chelugui (Vyama vya Ushirika), Zacharia Njeru (Ardhi) na viongozi wa kaunti ya Embu wakiongozwa na Gavana Cecily Mbarire.