NA MASHIRIKA
KAMPALA, UGANDA
RAIS wa Uganda, Yoweri Museveni amepimwa na kupatikana ana virusi vya corona.
Hata hivyo, afisa mkuu wa wizara ya afya amesema rais yuko katika afya njema na ataendelea na majukumu yake, huku akipata matibabu.
“Leo Rais alipimwa na matokeo yakawa ana virusi vya corona. Hii ilikuwa baada ya rais kuonyesha dalili za mafua. Licha ya hayo, yuko katika hali nzuri na anaendelea kutekeleza majukumu yake kama kawaida huku akizingatia Kanuni za Afya,” Dkt Diana Atwine, katibu mkuu katika Wizara ya Afya, amechapisha kwenye mtandao wa Twitter.
Isitoshe, mapema Jumatano baada ya kutoa hotuba ya taifa katika Majengo ya Bunge, Museveni, 78, alidokeza kwamba huenda alikuwa ameambukizwa virusi hivyo.
Aliongeza kwamba majira ya asubuhi, alihisi baridi kidogo, na ndipo akaomba madaktari wamfanyie vipimo vya corona.
Alisema vipimo viwili kati ya vitatu alivyofanyiwa vilileta matokeo ya kuwa yuko buheri wa afya bila kuwa na virusi vya corona huku akisubiri matokeo ya kipimo cha tatu na cha mwisho.
Katika hotuba yake, alisema alifika bungeni akitumia magari tofauti na yale ya mkewe ambaye ni Mama wa Taifa, Bi Janet Kataha, alitumia.
“Mimi nashuku nina virusi vya corona ninaposimama hapa. Ndio maana mmeniona nikija kwa kusafiria gari tofauti na mke wangu,” rais Museveni alisema.
Katika kilele cha janga la corona, Uganda ilikuwa na baadhi ya kanuni kali za kuzuia kusambaa kwa virusi hivyo barani Afrika.
Baadhi za kanuni hizo ni pamoja na amri ya kutotoka nje, kufungwa biashara na kufungwa kwa shule, kufungwa kwa mipaka miongoni mwa masharti mengine.
Vilevile, wakati wa janga hilo, rais Museveni, ambaye alikuwa amechanjwa, alionekana kila mara hadharani akiwa amevalia barakoa huku akifanya kazi zake rasmi.
Alionekana pia akikaa mbali na watu na mara nyingi alionekana ameketi peke yake kwenye hema lililowekwa kwenye nyasi nje ya ofisi yake wakati wa kukutana na wageni.
Kanuni za afya kuhusu matibabu ya corona zinasema ikiwa yeyoye ana maumivu ya kichwa, mafua, mwili kulegea, kupumua kwa shida na kuwashwa na koo, aone daktari.
Kando na hayo, rais Museveni hakuwa amevalia barakoa wakati alipokuwa akitoa hotuba yake kwa taifa.
Awali siku hiyo, kiongozi wa upinzani Uganda, Mathias Mpuuga alikuwa ameambia wanahabari kwamba serikali imetumia pesa nyingi za umma kulazimisha wale wote wanaokutana Rais Museveni kupimwa kwa lazima kubaini ikiwa wana virusi vya corona au la.