NA GEOFFREY ANENE
MWANATENISI Angella Okutoyi ameelezea kufurahishwa na jinsi mwaka 2022 umemwendea.
Akizungumza na Taifa Spoti baada ya kuwasili nyumbani jana kutoka Amerika, Okutoyi alisema sasa anatupia jicho mashindano ya wanawake ya dola 15,000 za Amerika (W15) jijini Nairobi.
“Nimepata matokeo mazuri na pia mengine yasiyo mazuri, lakini kwa jumla umekuwa mwaka mzuri kwangu tangu Januari. Nimepata mafanikio na uzoefu katika mechi za mchezaji mmoja kila upande na pia wachezaji wawili kila upande,” alitanguliza.
“Nafurahia kwa nafasi yangu nzuri kwenye viwango vya ubora vya Shirikisho la Kimataifa la Tenisi (ITF), nambari 49. Niko ndani ya 50-bora ambayo ndio nafasi yangu nzuri kabisa,” aliongeza Okutoyi.
Mkenya huyo alifika raundi ya tatu kwenye Grand Slam ya haiba ya chipukizi nchini Australia, raundi ya pili ya French Open, kushinda taji la wachezaji wawili Wimbledon na kufika raundi ya pili ya mchezaji mmoja na wachezaji wawili US Open.
Katibu wa Shirikisho la Tenisi Kenya, Wanjiru Mbugua, alisema ni furaha kuwa Okutoyi ameitiwa ufadhili wa katika taasisi za elimu ya juu nchini Amerika.