• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 5:55 AM
Alai na Sonko wavuana mashati mtandaoni

Alai na Sonko wavuana mashati mtandaoni

Na MWANDISHI WETU

MWAKILISHI wa wadi ya Kileleshwa Robert Alai amemsuta aliyekuwa gavana wa Nairobi Mike Sonko kwa kujinasa videoni akionyesha kitita cha pesa.

Sonko alijirekodi akionyesha kiasi cha pesa alichokuwa nacho nyumbani huku akiwaporomoshea matusi waliokuwa wamemkwaza.

Video hiyo iliyoenea mtandaoni, ilionyesha Sonko akifungua vitita vya pesa na kuringa nazo.

Hata hivyo, video hiyo iliyopata maoni tofauti kutoka kwa Wakenya, imemvutia Alai aliyesema, “Hata kama unaweza rekodi video ya pesa ulizo nazo haimaanishi wewe ni mtu mwenye busara. Unaweza kuwa na pesa nyingi lakini akilini wewe ni maskini. Jamani, tafuteni maarifa na hekima. Hakuna kitu kitakachokosa kusuluhishwa kwa mkutano.”

Sonko amtaka Alai kufyata ulimi

Sonko kwenye jibu lake lililokuwa na matusi alimweleza Alai kufyata mdomo na kushughulika na mambo yake.

“Maisha ni yangu. Yako ya MCA umesaidia nayo nani? Na bado ujue ninaweza msaidia mtu yeyote hata wewe kwani ulikuwa rafiki yangu hapo mbeleni. Mungu akikuchukua mbele yangu lakini hilo si ombi langu, nitahakikisha kuwa umezikwa kama mfalme. Mimi pamoja na kamati yako ya watakaokuwa wakipanga mazishi yako, tutauhifadhi mwili wako kwa wiki zingine tatu ili niweze kukujengea nyumba nzuri utakayopumzishiwa,” akasema.

Pesa hizo zilizokuwa zimefunganywa kwa dola na elfu moja, zilikuwa kwenye sanduku la dhahabu.

Sonko aliyeonekana kuwa na hasira aliwaeleza waliomghadhabisha kuwa yeye ni tajiri.

“Wacha nikuonyeshe pesa. Mtu lazima ajipange katika maisha haya. Hii yote ni milioni mbili ya mafuta. Pale pana zaidi ya milioni 50. Iwapo Mungu atakuchukua mbele yangu nitakununulia sanduku na kukusafirisha hadi Embu.

“Hii yote ni ya kununua mafuta. Wacha nitoe pesa zingine ili nikuonyeshe kuwa ninaweza watusi watu kesho asubuhi. Nani alikuambia kuwa watu huku Kenya hawana pesa? Wacha nitoe pesa zingine ili usifikirie ni ghushi,” akasema kwa video yake ya dakika tatu.

  • Tags

You can share this post!

Vurumai: Polisi waitwa kupanga wakazi waliofika kupokea...

Akothee na Jaguar wakabana koo kuhusu utajiri

T L