• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 5:07 PM
Kisura anayelenga kupata mavuno mazuri katika uigizaji

Kisura anayelenga kupata mavuno mazuri katika uigizaji

NA JOHN KIMWERE 

NI ndoto ya kila msanii kuona anaimarika katika kazi zake na kutambulika kote duniani.

Meegesh Neshiro almaarufu Chep kamwe haachwi nyuma licha ya pandashuka ambazo hupitia kwenye shughuli za uigizaji. Sura na sauti yake sio geni kwa wapenzi wa burudani ya maigizo nchini.

Anaorodheshwa kuwa ni miongoni mwa wasanii wanaokuja wakilenga kuendelea kuteka hadhira miaka ijayo.

Kando na uigizaji, hutengeneza mapambo ya aina tofauti ikiwamo vipuli vya masikio na mapambo ya nyumba kati ya mengine.

Tayari ni mwanafunzi wa mwaka wa nne kwenye Chuo Kikuu cha Kenyatta (KU) anakotarajia kuhitimu kwa shahada ya digrii kwenye masuala ya uigizaji.

”Nilianza kuvutiwa na masuala ya uigizaji nikiwa shule ya upili bila kufahamu babangu mzazi alikuwa stadi kwenye uandishi wa scripts,” amesema.

Ameongeza baadaye aliuliza mamake na kumfahamisha kuwa babake alikuwa msanii. Anashikilia kuwa ndani ya miaka mitano ijayo amepania kutimiza azma ya kuibuka mwigizaji wa kimataifa na kushiriki filamu nyingi na kupenya kupeperushwa kupitia runinga tofauti.

Binti huyu kitaaluma alianza kujituma kwenye masuala ya uigizaji akiwa chuo Kikuu mwaka wa kwanza 2019. Alifanya kazi na kundi liitwalo Igiza Arts Production. Kwa sasa amejizolea umaarufu zaidi kupitia kipindi kiitwacho Classmates akiigiza kwa jina Chepkoech. Classmates hupeperushwa kupitia runinga ya KBC.

Kwa ujumla msichana huyu kutoka eneo la Kirindom, Trans-mara anajivunia kufanya kazi na makundi kadhaa na kushiriki filamu tofauti ikiwamo: Ustadi Film (Rise of Phoenix, Wimped), Igiza Arts (Perishable Cherishable), Rising Star Production (The enemy of the state).

”Nilipata mtihani mgumu kushiriki filamu ya ‘Wimped’  lakini niliipenda sana ilinifanya kuelewa zaidi kuhusu masuala ya vurugu za wanaume dhidi ya wanawake (GBV),” akasema.

Kwa jumla anajivunia kushiriki filamu kibao ambazo zimefanikiwa kupata mpengo na kupeperushwa kupitia runinga kama KBC, KU TV na Honey TV.

Meegesh Neshiro almaarufu Chep. PICHA | JOHN KIMWERE

Anasema hutiwa motisha zaidi na historia na uigizaji wake msanii Taraji Penda Henson maarufu Cookie aliye mzawa wa Marekani.

Taraji alijizolea umaarufu mkubwa kupitia filamu zake ikiwamo ‘Empire,’ ‘What men want,’ ‘Baby boy,’ na ‘Hidden figures’ kati ya nyinginezo.

Binti huyu sio mchoyo wa mawaidha. Anashauri wenzie kuwa hakuna lisilowezekana bora kumakinika na kutia bidii wakipata nafasi.

”Jambo muhimu ni kwamba ukipata fursa jitume huonyeshe kazi yako ilivyo,” akasema.

Anasema kwa uigizaji angependa kufanya kazi na Sarah Hassan ilhali kwa wavunja mbavu wa humu nchini anapenda kuchapa shughuli na Awinja aliyekuwa akishiriki kipindi cha Papa Shirandula. Sarah Hassan anajivunia kushiriki kipindi cha ‘Crime and Justice’ pia ‘Zora’ ambacho hupeperushwa kupitia Citizen TV.

Kisura huyu anasema wanawake wanaoshiriki uigizaji hupitia pandashuka sio haba. Anadai mwigizaji anaweza akajaribu auditions takribani 20 na kupata nafasi moja ama kuambulia patupu.

  • Tags

You can share this post!

BORESHA AFYA: Fahamu ni kwa nini unafaa kunywa chai ya...

Sasa Academy yaibua warembo wembe katika voliboli

T L