• Nairobi
  • Last Updated December 3rd, 2023 7:00 PM
Bei ya pombe kuongezeka kwa asilimia 300 pendekezo la mbunge likipita

Bei ya pombe kuongezeka kwa asilimia 300 pendekezo la mbunge likipita

NA SAMMY WAWERU

MBUNGE wa Kenya Kwanza amependekeza nyongeza ya asilimia 300 kwa bei ya pombe na vileo vikali.

Bw Gabriel (GG) Kagombe, ambaye ni mbunge wa Gatundu Kusini, amesema kwamba athari za kuongezeka kwa gharama ya maisha zinapaswa kuhisiwa katika sekta zote.

Kulingana na mbunge huyo wa chama cha United Democratic Alliance (UDA), sio chakula na mahitaji muhimu ya kimsingi pekee yanapaswa kubeba mzigo wa kuongezeka kwa gharama ya bidhaa, akisema athari za mfumuko wa bei zinapaswa kusawazishwa kwa sekta zote.

Anasema, ustaarabu hasa unywaji pombe unapaswa pia kugharamika zaidi.

Kupitia kurasa zake za mitandao ya kijamii mnamo Ijumaa, Septemba 21, 2023, Bw Kagombe alisema kwamba serikali ya Rais William Ruto itapendekeza nyongeza kwa bei ya pombe na vinywaji vikali.

“Mazungumzo haya kuhusu gharama ya maisha yamezua tumbojoto. Kama serikali, sasa tutapendekeza kueneza athari za mfumuko wa bei katika sekta zote. Pombe ni mojawapo ya kitega uchumi kikubwa.

“Tunaweza kuongeza ukusanyaji ushuru hadi nusu trilioni kutoka Sh300 bilioni tunazokusanya sasa, kwa kuongeza mara tatu ya bei ya chupa ya bia, whisky, na divai,” mbunge huyo aliandika kwenye ukurasa wake rasmi wa Facebook.

Kwa mfano, alipendekeza kwamba bei ya chini ya chupa ya Tusker iwe Sh600, huku vinywaji kali kama vile Gin viuzwe Sh15, 000.

Kulingana na pendekezo la mbunge huyo wa UDA, kuongeza mara tatu bei ya pombe na vinywaji vikali kunamaanisha kuongeza bei kwa asilimia 300.

“Tutaona jinsi ya kujumuisha pendekezo hili kwenye Mswada wa Fedha,” Kagombe alieleza.

Mswada tata wa Fedha 2023 ulipitishwa mwaka huu na Bunge la Kitaifa na baadaye kutiwa saini kuwa Sheria na Rais Ruto.

Hata hivyo, Sheria hiyo ya Fedha, ambayo inapendekeza nyongeza ya kodi na ushuru kwa bidhaa muhimu za kimsingi, imepingwa kortini na upinzani, ukiongozwa na Seneta wa Busia, Okiya Omtatah, mashirika ya kutetea haki za kibinadamu, na vyama vya wafanyakazi.

Miezi michache baada ya Mswada huo kuwa Sheria, Wakenya tayari wameanza kuhisi athari za kupanda kwa gharama ya maisha, haswa kutokana na ongezeko la asilimia 8 hadi 16 la VAT ya mafuta.

  • Tags

You can share this post!

Mganga atisha kumdhuru mteja aliyeshindwa kukamilisha...

Programu ya kutatua migogoro kidijitali yazinduliwa nchini

T L