• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 5:55 AM
FAUSTINE NGILA: Jihadhari na matapeli wa sarafu za kidijitali

FAUSTINE NGILA: Jihadhari na matapeli wa sarafu za kidijitali

Wataalamu wakagua uvunaji wa bitcoin katika kituo cha Bitfarms eneo la Saint Hyacinthe, Quebec, Canada hapo zamani. Bitcoin ni sarafu ya kidijitali inayokubalika kama mbinu ya malipo kote duniani, na ndiyo sarafu kongwe zaidi ya kidijitali duniani. Picha/Maktaba

Na FAUSTINE NGILA

Katika kipndi hiki cha mahangaiko kutokana na athari za janga la corona, nimepokea malalamishi mengi kutoka kwa Wakenya kuhusu jinsi wamelaghaiwa mamilioni ya pesa wanapojaribu kuwekeza katika sarafu za kidijitali.

Ni mwaka jana tu ambapo mwanafunzi katika Chuo Kikuu cha Makerere nchini Uganda alipojitia kitanzi baada ya kupoteza Sh500,000 katika kipochi cha dijitali, na kuibua swali la ni hadi lini wawekezaji wataendelea kupunjwa kutokana na ukosefu wa maarifa kuhusu sarafu kama Bitcoin, Ethereum, Dogecoin, Ripple na Tether.

Soko zima la sarafu za kidijitali nchini limekumbwa na changamoto za ugumu wa kueleweka na mfumko wa thamani yake usioweza kubashiriwa. Lakini ripoti iliyotolewa wiki iliyopita na kampuni ya Mastercard inaonyesha kuwa asilimia 40 ya Wakenya wako tayari kuwekeza katika majukwaa haya hata ingawa hawana elimu inayohitajika.T

atizo kuu la vijana wa humu nchini ni kwamba wana tamaa ya kuitwa mabwanyenye katika kipindi cha muda mfupi, na ndiyo maana wanawekeza pesa bila kuelewa mbinu bora ya kufanya hivyo, na kuishia kupoteza kila kitu.Ripoti ya Citibank inaonyesha kuwa Kenya ni miongoni mwa mataifa ya Afrika yanayomiliki idadi kubwa ya sarafu za dijitali.

Utafiti mwingine wa Paxful unafichua kuwa katika kipindi cha corona, Wakenya waliwekeza zaidi kwenye sarafu hizi, kima cha Sh5 bilioni.

Nilipomtembelea Bi Beatrice Wanjiru katika mkahawa wake mjini Nyeri ambao unakubalia malipo ya sarafu za dijitali kama Bitcoin, Bitcoin Cash na Dash, niling’amua kuwa vijana wa mijini hawaelewi maana ya sarafu za kidijitali.

Alikiri kuwa kwa wakati mmoja, pia yeye alipoteza Bitcoin za thamani ya Sh500,000 kwenye tukio la wizi mtandaoni, wakati ulingo huo ulipokuwa ungali mpya nchini.

Ni kutokana na wizi huu ambapo benki kuu za Kenya, Uganda, Tanzania, Malawi, Zimbabwe, Nigeria na Afrika Kusini zimewaonya raia wao dhidi ya kuwekeza katika sarafu hizi kwa kuwa “hakuna usalama wowote mitandaoni na majukwaa hayo hayajadhibitiwa na serikali”.

Nikimhoji afisa mkuu mtendaji wa kampuni ya Amerika, Paxful inayoeneza elimu ya sarafu hizi duniani, Bw Ray Youssef, alisema ni hatua nzuri kwa mataifa hayo kutahadharisha raia dhidi ya kuwekeza kwenye biashara wasiyoielewa.

Ni wazi kuwa wakati wafanyabiashara wa mitandaoni wanapoteza hela zao kutokana na udukuzi, serikali hupatwa na hofu.Hata hivyo, watu wengi wanaopoteza fedha zao ni wale wazembe wasiopenda kusoma wala kutafiti kuhusu jambo baada ya kulisikia.Wengi ni wale wa tabaka la kati na juu wenye hela za ziada, lakini kukosa juhudi za kujielimisha kumewaponza.

Jihadhari na matapeli wa sarafu za kidijitali, mwanzo ujue kuna zaidi ya sarafu 9,000 kote duniani. Kuna zile za hakika na nyingine hewa ambazo zitakuhadaa kuwa zina thamani kisha kuporomoka baada ya wiki chache.

Hufai kuisubiri serikali au kampuni yoyote ile ikuelimishe kuhusu masuala haya, unafaa kujielimisha mwenyewe kwani taarifa za kuaminika ziko mitandaoni bila malipo.Kukosa kufanya hivi kutakuletea balaa. Utaendelea kulaghaiwa hela ulizosaka kwa jasho jingi, na kujutia kwa nini hukuwekeza muda wako katika kuelewa mwanzo unachokifanya.

Usiwasikilize wenzio wakidai hela haziwezi kuibwa kwenye kipochi cha dijitali, chukua muda wako na kutafiti ni kwa nini watu wengi wamepoteza nywila za akaunti zao na kupoteza hata mabilioni ya pesa.

You can share this post!

KENYA HIGH JUU

Wachina wabadilisha mwelekeo na kufuatilia zaidi lugha za...