• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 12:58 PM
FAUSTINE NGILA: Wapi utekelezwaji wa Ripoti ya Blokcheni?

FAUSTINE NGILA: Wapi utekelezwaji wa Ripoti ya Blokcheni?

Na FAUSTINE NGILA

NI miaka mitatu sasa tangu Ripoti ya Blockcheni na Akili Bandia (AI) iwasilishwe kwa serikali kwa ajili ya utekelezaji katika miradi ya kitaifa.

Lakini hakuna chochote Wizara ya Teknohama imeambia wananchi tangu ipokee ripoti hiyo ambayo ilipigiwa upatu kubadilisha utendakazi katika sekta za umma na kibinafsi nchini.

Ingawa suala la Blokcheni lingali geni kwa Wakenya wengi, serikali haijafanya lolote kueleza wananchi maana yake na umuhimu wake kwa taifa hili.

Kwenye mapendekezo ya ripoti hiyo, wanajopo wa Tume ya Blockcheni waliirai serikali itumie teknolojia hiyo katika sekta za afya, ardhi, fedha na elimu, lakini mafunzo na warsha kuhusu matumizi yake bado hazijaandaliwa.

Kufikia mwaka huu, Wakenya wanafaa kuwa na uelewa wa ndani kuhusu jinsi teknolojia hii inaboresha huduma, kwanza kwa kuzima ufisadi na kuwanasa wanaoiba fedha za umma.

Tunaelekea msimu wa siasa na hatimaye Uchaguzi Mkuu mwaka ujao, lakini wananchi hawana habari kuwa teknolojia ya blockcheni ina uwezo wa kuzima wizi wa kura na kuwafungia nje wanasiasa na wapigakura feki.

Hii ni teknolojia muhimu ambayo ina uwezo wa kuzima ghasia za baada ya kila uchaguzi, kwa kuitumia katika mchakato mzima wa kupiga kura, kuzihesabu na kutangaza mshindi.

Ni uvumbuzi wa kisasa ambao unawazuia wadukuzi ambao hunuia kuiba pesa au data za siri za watu, kampuni na serikali kwa kuwa unatambua kila mtu anayeingia mle ndani na kumwanika kwa umma papo hapo.

Iwapo wananchi watafahamishwa kuuhusu, utaweza kutumiwa kusimamia na kufuatilia matumizi ya fedha za serikali hadi kwenye kaunti, hali ambayo itawaogopesha wezi.

Tatizo la wizi wa fedha za kaunti hutokana na hali kwamba hela hizo hutolewa kutoka Hazina Kuu ambapo huibwa kabla ya kufikia serikali za kaunti litasuluhishwa na teknolojia hii.

Kila kaunti inaweza kugawiwa hela zake na kufuatiliwa kidijitali.Itakomesha mazoea ya wanasiasa kutumia wahasibu kuiba pesa kisha kufuta rekodi za wizi huo ili kuficha ushahidi.

Pia, mtindo wa baadhi ya wafanyabiashara na kampuni kukwepa kulipa ushuru utaisha huku rekodi za Blockcheni zikitumika kortini kuhukumu mafisadi.Lakini mbona mswada haujatua bungeni kujadili jinsi blockcheni itatumika, miaka mitatu baadaye?

Mbona serikali imenyamazia ripoti hiyo?Yamkini uroho na ubinfasi wa wanasiasa na washauri wa serikali ndio kikwazo kikuu katika mpango mzima wa kufumbia macho teknolojia yenye uwezo mkubwa.Labda wanajiuliza, tukitekeleza hii blockcheni tutaiba hela za umaa vipi? Tutanyakua mashamba vipi?

Tutaiba kura vipi? Tutatoa rushwa vipi?Yaani, kimsingi, wanasiasa walio serikalini wanaonekana kuigomea teknolojia hii kwa kuwa itawakata miguu, itawaondoa kwenye utafunaji wa mabilioni ya walipa ushuru, itawafilisisha!

Ni mwenendo ambao unafaa kukoma, na kila mfanyakazi wa serikali kuzoea kujizolea mali kwa njia halali. Bila hili, ripoti ya blockcheni itasalia tu kwa maktaba ya serikali ambapo kwa sasa inalamba vumbi.

You can share this post!

Uhuru sasa kuzuru Ukambani

Sindwele amtoroka dereva wake kutokana na ‘uchochole’