NA MAGDALENE WANJA
Je, ushawahi kufahamu manufaa ya kuwa mkwasi katika matumizi ya mitandao? Kijana Gesora Mwasi alianza kuvuna hela nzuri akiwa Mwaka wa Kwanza tu chuoni kutokana na utaalamu wake wa kunadi bidhaa na huduma kupita mitandao.
Alikuwa ametengeneza ufuasi mkubwa katika ukurasa wa Facebook, wa zaidi ya wachangiaji 20,000.
Hata hivyo, aliamua kuuza ukurasa huo muda mfupi baadaye.
“Niliuza ukurasa huo kwa Sh10,000 ambazo zilikuwa pesa nyingi sana wakati huo, ikizingatiwa kwamba nilikuwa mwanafunzi,” anasema Gesora.
Huo ndio ulikuwa mwanzo wa kufanya biashara mtandaoni kuimarisha mauzo.
Akajitosa kwa biashara ya kuwatangazia wenye biashara, wenye kupanga sherehe na matukio ya biashara tofauti tofauti.
Alipokamilisha masomo yake katika Chuo Kikuu cha Strathmore, aliamua kuipanua biashara hiyo kwa kiwango kikubwa zaidi.
“Wakati huo, nilikuwa na mapato mazuri kutokana na biashara hiyo,” akasema Gesora.
Baadaye ya muda mfupi, aliungana na marafiki wawili ili kupanua biashara hiyo, ila haikudumu kwa muda mrefu kutokana na tofauti za maono.
Kutokana na akiba aliyokuwa ameweka ya Sh40,000 aliamua kufanya biashara upya tena, ila haikuwa rahisi katika siku za mwanzo.
“Mteja wa kwanza aliyenifungulia awamu hii mpya, alikuwa na biashara katika hoteli moja ya kifahari katika eneo la Westlands jijini Nairobi,” akasema Gesora.
Hiyo ilifuatiwa na biashara nyingi ambazo zilimpa nafasi ya kujifunza mengi katika sekta hiyo.
Kufikia sasa, biashara hiyo ina uwezo wa kuwahudumia wateja zaidi ya 50 kila mwezi, na ina wafanyakazi 250.
Gesora anaongeza kuwa anatumai ataweza kuipanua biashara hiyo zaidi.