NA RICHARD MAOSI
ANNABEL Mideva atawakilisha Kenya katika michuano ya kimataifa ya mchezo wa sataranji mnamo Aprili 13, 2023 katika taifa la Ugiriki.
Hii haitakuwa mara ya kwanza kwa kinda huyu kuwakilisha taifa kwenye michuano ya haiba kubwa ndani na nje ya Kenya.
Kwa mujibu wa Mideva, alianza kupenda chess alipokuwa akimuona babake akicheza nyumbani kila siku ndiposa akapata hamu ya kujifunza hatua kwa hatua.
“Nilipoanza kushiriki, ilikuwa ni njia mojawapo ya kuburudika lakini nilijitosa mchezoni kwa asilimia mia moja baada ya kumuona kaka yangu mdogo akituzwa medali,” akasema.
Mnamo 2021, Mideva alipata fursa ya kutangamana na mchezaji mahiri wa chess, Ben Magana, kwenye mchuano wa Nakuru Open Tournament.
Anasema alivutiwa sana na weledi wa nguli huyu kiasi kwamba alitamani kuwa ingetokea siku ambayo wawili hawa watachuana katika jukwaa moja, ikizingatiwa kuwa fursa kama hii hutokea kwa tukizi mno.
Ili afi kie kiwango cha kutopea, alijiunga na Chuo cha Nakuru Chess Academy na akaanza kujinoa taratibu akiamini kuwa siku moja angekuja kuwa mchezaji wa kutajika.
Alikuwa chini ya mkufunzi Dickson Gitari ambaye amekuwa akinoa kipaji chake mpaka sasa. Vilevile, Gitari amefanikisha juhudi za wachezaji wake wengi kufanya vyema mchezoni.
Mchuano wa kwanza kwa Mideva kushiriki ni Novemba 2021 ambapo aliibuka wa tano, hali ambayo ilimpatia motisha akaendelea kujipiga msasa na hadi sasa hakuna mchezaji ambaye amewahi kumshinda kwenye kitengo chake.
Alishinda mchuano wa Kenya National Junior Chess Championship uliofanyika jijini Mombasa mnamo 2022, hali ambayo ilimfanya kushiriki kwenye ulingo wa bara la Afrika nchini Zambia.
Anaungama kuwa atakumbana na ushindani mkali nchini Ugiriki lakini ana uhakika kuwa atashinda kwenye michuano yake yote, ikizingatiwa kuwa amefanya mazoezi ya kutosha.
Ushauri wake kwa wale wanaoibukia kwenye mchezo wa chess ni wajiwekee malengo na kumtafuta mkufunzi ambaye atawasaidia kunoa makali yao.
Kwa Mideva, mchezo wa chess ni sehemu ya maisha yake kwani utamkuta akifanya mazoezi na kaka yake mdogo kila wakati nyumbani.
Kwa upande mwingine, babake Bw Winson Makanga anasema kuwa anajivunia juhudi za mwanawe, na akiwa mchezaji wa chess vilevile anaona kuwa amempokeza binti yake mikoba ya kuendeleza mchezo wenyewe.
Aliongezea kuwa nia yake kuu ni kumsaidia binti yake katika kila hali ili afi kie kiwango cha kuitwa mwalimu wa walimu katika mchezo wa sataranji.