NA CHRIS ADUNGO
UANAHABARI ni taaluma ambayo Selly ‘Kadot’ Amutabi alianza kuvutiwa nayo katika umri mdogo.
Alianza safari ya elimu akifahamu thamani ya Kiswahili na umuhimu wa vyombo vya habari.
Wazazi walimruhusu ajiunge na makundi mbalimbali ya uimbaji na uigizaji kanisani; nao walimu waliomlea kiakademia wakampa fursa tele za kushiriki mashindano ya ngazi na viwango tofauti kwenye fani ya drama.
Baada ya kutambua kipaji chake cha uanahabari, Selly alitia azma kukipalilia. Alitegemewa sana kutumbuiza wazazi na wageni kwa nyimbo, maigizo na densi nyakati za hafla na mikutano muhimu shuleni.
Majukwaa hayo yalinoa kipaji chake cha ulumbi na ‘sauti yake ya utangazaji’ ikamfanya kuwa maarufu miongoni mwa wanafunzi wenzake.
Selly alizaliwa katika eneo la Emuhaya, Kaunti ya Vihiga na akakulia katika mitaa ya Kimumu, Beta Farm na Pioneer iliyoko Eldoret, Kaunti ya Uasin Gishu.
Ndiye mwanambee katika familia ya watoto watano wa Prof Maurice Amutabi na mwalimu Violet Locho.
Alisomea katika chekechea za Tiny Tots na Hill School mjini Eldoret kabla ya kujiunga na shule za msingi za Kimalel (Eldoret) na St Anne’s Girls Mumias (Kakamega) kisha shule ya upili ya Bunyore Girls (Vihiga).
Ingawa matamanio yake mengine yalikuwa kuwa rubani au wakili, alisomea uanahabari katika Chuo Kikuu cha Daystar (2008-2012). Akiwa huko, alihudumu katika redio ya Shine FM na akapanda ngazi kuwa mkuu wa kituo hicho kinachomilikiwa na Chuo Kikuu cha Daystar.
Alishiriki mafunzo ya nyanjani katika Ghetto Radio 89.5 FM mwanzoni mwa 2012 na akahamia baadaye katika idhaa ya Kiswahili ya BBC iliyomwaminia kutangaza taarifa za michezo.
Selly aliajiriwa na Nation Media Group (NMG) mnamo 2013 na akawa mwendeshaji wa kipindi cha kila alfajiri, ‘Tambira’, katika iliyokuwa redio ya QFM.
Kufungwa kwa idhaa hiyo mnamo 2016 kulimpa jukwaa mwafaka la kujitosa kikamilifu katika fani ya muziki na akajikuza zaidi kisanaa akiwa na kundi maarufu la Afrizo Band.
Alipata pia nafasi maridhawa ya kushirikiana kikazi na baadhi ya waimbaji wa nyimbo za injili wa humu nchini kwa lengo la kueneza Ukristo na kuwaelekeza wanafunzi kimaadili.
Isitoshe, alijiendeleza kimasomo kwa kujiunga na Chuo Kikuu cha USIU-A mnamo 2017 kusomea shahada ya uzamili katika masuala ya kidiplomasia na mahusiano ya kimataifa.
Ilikuwa hadi 2018 ambapo Selly alirejea katika ulingo wa uanahabari baada ya kuajiriwa na Qwetu Radio. Alihudumu huko kwa kipindi kifupi kabla ya kutwaliwa na Royal Media Services (RMS) kuwa mtayarishaji wa vipindi mbalimbali vya Radio Citizen kuanzia Agosti 2018.
Mbali na kuwa nahodha wa ‘Wingu la Baraka’, amekuwa pia akishirikiana na Mzazi Willy M Tuva kuendesha kipindi ‘Mambo Mseto’ tangu 2019.
Aliwahi pia kujaza pengo la mwanahabari Jeff Koinange mnamo 2020 katika kipindi ‘Hot Breakfast’ kwenye Hot 96 FM.
Zaidi ya uanahabari, Selly pia ni mhamasishaji wa afya ya akili huku akishiriki miradi anuwai ya kushughulikia waathiriwa wa ugonjwa wa fistula.
Kutokana na ubunifu wa kiwango cha juu na weledi wake kukisarifu Kiswahili kwa ufundi mkubwa, Selly pia hupata fursa adhimu za kuwa mvumishaji wa bidhaa mitandaoni na mfawidhi wa sherehe muhimu za watu binafsi, mashirika, kampuni na idara mbalimbali za serikali.
Zaidi ya kukuza na kulea vipaji vya wanahabari chipukizi, maazimio yake mengine ni kuwa miongoni mwa wadau wakuu wenye uwezo wa kutoa maamuzi muhimu katika tasnia ya uanahabari nchini Kenya.
“Kufaulu katika uanahabari kunahitaji mtu kuwa na msukumo, ari na mshawasha wa kushiriki mafunzo yatakayomkuza kitaaluma. Kipende na uthamini unachokifanya. Tanguliza Mungu katika kila hatua, jiamini na ujitume bila kutamauka,” anashauri.
Selly anaistahi sana familia yake inayozidi kuiwekea kazi yake mshabaha na thamani kubwa. Mumewe mpendwa ni Dkt Matibe.
Subscribe our newsletter to stay updated