Na CHRIS ADUNGO
MATAMANIO makubwa ya Nelson Mandela, 34, ni kutikisa ulingo wa filamu kimataifa kiasi cha kufikia kiwango cha staa wa Scotland, Gerard James Butler.
Zaidi ya kufyatua michezo inayokubalika kimataifa na kumiliki kituo cha sanaa kitakacholea vipaji vya waigizaji chipukizi, analenga pia kuwa mshereheshaji stadi na mlumbi wa kustahiwa.
Anayezidi kuweka hai ndoto zake na kumchochea pakubwa kisanaa kutoka humu nchini ni Bw Suleiman Fadhili anayeamini kuwa uigizaji – ambao zamani ulitumika sana kwa ajili ya burudani pekee – sasa ni kazi ya kitaaluma katika soko pana la ajira ulimwenguni.
“Ni sanaa inayotupa fursa ya kuthamini tamaduni mbalimbali, kupitisha elimu, kukuza maadili, kubainisha taratibu za maisha na kuchangia ubidhaaishaji wa lugha,” anashadidia.
Mandela alizaliwa Lamu na akalelewa katika eneo la Shimo La Tewa, Kaunti ya Mombasa. Ndiye wa nne katika familia ya watoto saba wa Bi Tabitha Sidi na marehemu Bi Andrew Sabastian Odera.
Alisomea katika shule ya msingi ya Shimo La Tewa (1994-1997) kabla ya kujiunga na shule ya msingi ya Bamburi, Mombasa (1998-2002) kisha shule ya upili ya Serani, Mombasa (2003-2006). Ana stashahada ya usimamizi wa masuala ya forodha kutoka Bandari Institute, Mombasa (2007-2009).
Alijitosa katika uigizaji mnamo 2009 na akapata fursa ya kunogesha kipindi ‘Majaliwa’ (Citizen TV) akiigiza mhusika Kito. Filamu hiyo ilikuwa yake ya kwanza runingani na ndiyo ilimkweza zaidi katika ulingo wa uigizaji.
Kiwango chake cha juu cha ubunifu kilivutia vinara wa Voyager Beach Resort waliomwajiri kusimamia kundi la wasanii wa kutumbuiza wageni kila jioni katika mkahawa huo wa kifahari jijini Mombasa.
Zaidi ya kukoleza mapenzi yake kwa muziki, kazi hiyo aliyoifanya kati ya 2010 na 2016, ilimkuza zaidi kisanaa na kumpa jukwaa mwafaka la kujifunza kuwa DJ kuanzia 2012.
Maarifa yake yaliwaniwa baadaye na wamiliki wa Pride Inn Beach Resort na akapata fursa ya kuwa msimamizi mkuu wa kitengo cha burudani katika hoteli hiyo iliyoko Shanzu, Mombasa. Alihudumu huko kati ya Disemba 2016 na Disemba 2018.
Alitekeleza majukumu yake kwa urahisi kutokana na kipawa cha ulimi. Mandela ni mwepesi wa kutema maneno ya kuvunja mbavu kwa ufundi mkubwa.
Ndoto ya kuwa mjasiriamali wa kujitegemea ilianza kumtambalia 2018 na akaanzisha kampuni ya ‘Wezesha Consultancy’ inayojishughulisha na masuala ya burudani, uvumishaji wa huduma na bidhaa na uratibu wa hafla za sampuli tofauti.
Mandela amewahi kupata fursa adhimu za kusimamia mahamasisho ya kuhimiza utangamano katika ngazi na viwango mbalimbali. Aidha, yeye huwa mfawidhi wa sherehe muhimu za watu binafsi, mashirika, kampuni na idara mbalimbali za serikali.
Ufanisi huo ni zao la kipaji chake cha ulumbi, weledi wa kusarifu lugha, upevu wa masimulizi katika maigizo na ujuzi wa kusuka na kuremba maneno.
Baada ya kushiriki mchezo ‘Maza’ (Maisha Magic East – DStv) mnamo 2019, milango ya heri ilijifungua zaidi na Mandela akanogesha ‘Kovu’ (Maisha Magic East). Kwa sasa anaigiza mhusika Kokan katika mchezo ‘Sultana’ (Citizen TV).
Subscribe our newsletter to stay updated