NA CHRIS ADUNGO
ZAIDI ya kutoa fursa kwa washiriki kujadili kwa jicho la kiuhakiki nafasi ya Kiswahili katika uchumi wa kijani, Kongamano la 23 la Kimataifa la Chama cha Kiswahili cha Taifa (CHAKITA) mwaka huu 2023 liliwapa pia wanachama jukwaa la kuchagua viongozi wapya.
Kongamano hilo la siku mbili lilifanyika katika Chuo Kikuu cha Kabianga, Kaunti ya Kericho, kati ya Machi 1-2, 2023, na lilileta pamoja mamia ya wajumbe kutoka Kenya, Tanzania, Uganda, Rwanda na Burundi.
Dkt Fred Simiyu wa Chuo Kikuu cha Kibabii, Kaunti ya Bungoma, alitwaa mikoba ya uenyekiti wa CHAKITA kutoka kwa Profesa Mark Mosol Kandagor aliyehudumu katika wadhifa huo kuanzia 2017.
Mbali na kushikilia nafasi hiyo muhimu katika mojawapo ya asasi za juu zaidi za ukuzaji wa Kiswahili ndani na nje ya Kenya, Prof Kandagor aliwahi pia kuwa Mkuu wa Idara ya Kiswahili na Lugha Nyingine za Kiafrika katika Chuo Kikuu cha Moi, Eldoret (2012-2019).
Amekuwa Mhariri Mkuu wa Chama cha Kiswahili Afrika Mashariki (CHAKAMA) tangu 2015; mjumbe katika Bodi ya Chama cha Ukuzaji wa Kiswahili Duniani (CHAUKIDU) kuanzia 2020; na Mtiva Mshiriki (Associate Dean) wa Kitivo cha Sanaa na Sayansi za Jamii katika Chuo Kikuu cha Moi tangu 2021.
“Akademia ni uwanja unaowaweka wahusika katika ulazima wa kusoma kwa mapana, kuandika makala, kutunga vitabu, kuhudhuria makongamano na kuwasilisha makala katika vikao vya ngazi na viwango mbalimbali,” anatanguliza.
“Majukwaa ya sampuli hii huwapa wasomi fursa maridhawa za kujifunza kuongoza na kupokezana uongozi huo kadri wanavyoshirikiana kusambaza maarifa na kutoa mchango wao katika utafiti, uandishi na ufundishaji wa taaluma anuwai,” anaelezea.
Sifa za uongozi zilianza kujikuza ndani ya Kandagor katika umri mdogo. Asipokuwa darasani, huwa anatumia ujuzi wake wa ualimu kuipa jamii mwelekeo. Ni mchungaji mshiriki wa Kanisa la Pioneer Community mjini Eldoret aliye na jukumu la kulea na kukuza vijana kimaadili.
Baada ya kukamilisha KCSE, alijiunga na Chuo Kikuu cha Mashariki mwa Afrika Baraton (UEAB) kusomea shahada ya B.A (Kiswahili na Kiingereza) kati ya 1993 na 1997.
Alifundisha Kiswahili katika shule ya upili ya Lake Bogoria, Kaunti ya Baringo, kwa mwaka mmoja kabla ya kujiunga na Chuo Kikuu cha Nairobi kusomea shahada ya uzamili (M.A Kiswahili) katika Idara ya Isimu na Lugha za Kiafrika (1998-2000).
Mnamo 2001, Kandagor aliteuliwa kuwa Mwalimu Mkuu wa kwanza wa shule ya upili ya AIC Ebenezer iliyoko Kabarnet, Baringo. Alihudumu huko kwa miaka minne hadi 2004 alipoajiriwa kuwa Mhadhiri wa Kiswahili katika Chuo Kikuu cha Kenya Methodist (KeMU) mjini Meru.
Alihamia katika Chuo Kikuu cha Moi kuwa mhadhiri wa kozi za taaluma za Isimu na Isimujamii mnamo 2007 na akaanza kusomea shahada ya uzamifu (PhD) aliyoihitimisha 2011 kwa uelekezi wa Prof Issa Mwamzandi na marehemu Prof Naomi Luchera Shitemi.
Kandagor alizaliwa mwaka wa 1974 katika eneo la Marigat, Baringo. Alianza safari ya elimu katika shule ya msingi ya Marigat kabla ya kujiunga na shule ya upili ya Marigat. Aliyempigia mhuri kuwa mtaalamu wa Kiswahili ni mwalimu Caleb Ong’ong’a aliyempokeza malezi bora ya kiakademia katika shule ya upili.
Vyombo vya habari, mitandao ya kijamii na uandishi wa vitabu ni majukwaa mengine ambayo Prof Kandagor hutumia kushiriki mijadala ya kitaaluma. Kufikia sasa, anajivunia zaidi ya machapisho 70 katika vitabu na majarida rasmi ya kitaaluma na amehariri zaidi ya vitabu 10.
Subscribe our newsletter to stay updated