NA WANDERI KAMAU
WENYEJI wa Mlima Kenya sasa wako kwenye njia panda, baada ya Naibu Rais Rigathi Gachagua kusema kuwa ameanza kupata changamoto katika juhudi za kulainisha sekta ya kahawa na majanichai.
Ikizingatiwa kuwa idadi kubwa ya wenyeji walimchagua Bw Gachagua na mrengo wa Kenya Kwanza kwa ahadi ya kufufua sekta ya kilimo, inayojumuisha ukuzaji wa mazao kama pareto, miraa na ufugaji ng’ombe wa maziwa, wadadisi wanasema kuwa Bw Gachagua alikosea sana kukubali kwamba ameanza kupata changamoto katika juhudi za kulainisha sekta hiyo muhimu.
Kwenye mahojiano na kituo kimoja cha televisheni Desemba, Bw Gachagua aliwaahidi wenyeji wa Mlima Kenya kumpa siku sitini pekee, ambapo wangeanza “kuona matunda ya vita vyake dhidi ya mitandao hiyo”.
“Nipeni siku sitini pekee. Nitaanza kuwafuata watu hao unyo unyo bila kuwaogopa. Hatutakubali wakulima wetu kunyanyaswa tena. Unyanyasaji huo lazima ufike mwisho,” akaapa Bw Gachagua.
Lakini Ijumaa, Bw Gachagua alisema anahitaji maombi kwani mitandao hiyo ina nguvu kuliko alivyofikiria.
“Sekta za kahawa na majanichai bado hazijaimarika. Vita hivi ni vikubwa sana. Nawarai muniombee Mungu ili watu hao wasije kunidhuru kwa sababu ni watu wabaya. Ni watu watano. Wameungana pamoja ili kudhibiti soko kuu la kuuzia mazao hayo mawili (jijini Mombasa). Wamekubaliana kuhusu utaratibu ambao huwa wananunua mazao hayo na kuyasafirisha kwenye masoko bila kumruhusu mtu mwingine kuingilia sekta hizo. Huwa wanazungukana,” akasema.
Hata hivyo, alisema kuwa lazima afanye kila awezalo kuhakikisha kuwa wakulima wa mazao hayo wameanza kuyasafirisha nje ya nchi wao wenyewe na kuyauza moja kwa moja katika masoko tofauti duniani.
Kutokana na matamshi hayo, wadadisi wanasema kauli hiyo itakata kuwili kwa mustakabali wa kisiasa wa Bw Gachagua katika ukanda huo.
Kulingana na mdadisi wa siasa Kipkorir Mutai, Bw Gachagua alifanya kosa kubwa, kwani huenda tukaanza kushuhudia upinzani kutoka kwa wakosoaji wake.
“Ijapokuwa Bw Gachagua amekuwa akijisawiri kama msema kweli, alifanya kosa kukubali anakumbwa na changamoto kuwakabili watu ambao wamekuwa wakidhibiti sekta muhimu kama kahawa na majanichai. Ni kauli itakayokaribisha na kufungua upinzani ambao ameanza kushuhudia katika ngome yake ya Mlima Kenya,” akasema Bw Mutai.
Licha ya kusisitiza kwamba baadhi ya ajenda yake kuu ni kuwaunganisha wenyeji Mlimani, Bw Gachagua anaonekana kuanza kupata upinzani kutoka kwa mbunge Ndindi Nyoro (Kiharu).
Baadhi ya wanasiasa wamekuwa wakimsifu Bw Nyoro kama kiongozi anayefaa zaidi kumrithi Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta kama kiongozi na msemaji wa ukanda huo.
Kwenye mahojiano na ‘Jamvi la Siasa’, baadhi ya wazee walisema kuwa changamoto ambazo zimeanza kumkumba Bw Gachagua zinatokana na kutokuwepo kwa mchakato rasmi wa kumkabidhi uongozi kutoka kwa Bw Kenyatta.
“Suala lolote linalohusu uongozi wa jamii lazima liwashirikishe wazee. Ilivyo sasa, uongozi wa Mlima Kenya bado uko mikononi mwa Bw Kenyatta. Tangu jadi, taratibu za kumwapisha kiongozi mpya wa kijamii katika Mlima Kenya huhusisha wazee. Ikiwa hilo halijafanywa, basi hakuna mtu yeyote anayefaa kujitangaza kama kiongozi ama msemaji wa jamii,” akasema mzee mmoja kutoka Baraza la Wazee wa Jamii ya Agikuyu (KCE) ambaye hakutaja kutajwa.
Wadadisi wanasema ikiwa Bw Gachagua ataendelea kutoa kauli kama hizo kwenye majukwaa tofauti, basi huenda akajikwaa mapema yeye mwenyewe kwenye juhudi za ‘kuukomboa’ Mlima Kenya.
Subscribe our newsletter to stay updated