NA BENSON MATHEKA
TANGU ufichuzi wa kiongozi wa Azimio la Umoja One Kenya Raila Odinga kwamba huenda alishinda urais katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2022, Rais William Ruto ameonekana kumwandama wazi mtangulizi wake Rais mstaafu Uhuru Kenyatta.
Katika kile kinachotajwa kama kulipiza kisasi kufuatia uhasama wao katika utawala wa chama cha Jubilee na rais huyo mstaafu kumuunga Bw Odinga katika uchaguzi mkuu, Rais Ruto na washirika wake wanamlaumu Kenyatta na familia yake kwa kufadhili mikutano ya Azimio “ili wasilipe ushuru na kwamba atahakikisha hakuna anayetumia mamlaka yake kukwepa kulipa ushuru.”
Wadadisi wa siasa wanasema hatua ya Rais Ruto ilinuiwa kuzima mjadala kuhusu ufichuzi wa Bw Odinga ambao kufikia sasa tume huru ya uchaguzi na mipaka (IEBC) na wakereketwa wa muungano wa Kenya Kwanza hawajazungumzia.
“Walichoamua kufanya ni kubadilisha umakinivu wa Wakenya kwa kuzua madai kwamba Bw Kenyatta anafadhili mikutano na maandamano ya Azimio na madai ya kukwepa kulipa ushuru. Kwa ufupi, waliamua kumwandama Bw Kenyatta na familia yake na kwa kiwango fulani wakafaulu kuzima mdahalo kuhusu ufichuzi wa Bw Odinga,” asema mchambuzi wa siasa Dkt Isaac Gichuki.
Hata hivyo, inaonekana Bw Odinga anazidisha presha dhidi ya serikali kwa kuendelea na mikutano yake kote nchini. Mbali na madai hayo, serikali ilipunguza walinzi wa mtangulizi wake hatua ambayo pia ilizua mdahalo mkali.
Rais Ruto pia amenyakua wabunge 30 wa chama cha Jubilee ambacho kinaongozwa na Bw Kenyatta hatua ambayo inasemwa kuwa ya kumtoa pumzi kisiasa rais huyo mstaafu ambaye ni mwenyekiti wa Baraza Simamizi la Azimio.
Hatua hii inanuiwa kupunguza nguvu za Kenyatta hasa kwa kutishia kuchunguza mali na biashara za familia yake na kudhoofisha muungano wa upinzani ili kuacha viongozi wake bila wanajeshi wa kuunga maasi yao dhidi ya serikali. Kulingana na mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Nairobi Profesa Herman Manyora Uhuru hana cha kupoteza hata wabunge wa Jubilee wakijiunga na serikali.
“Hakuna yeyote Kenya anayeweza kuwa mjinga kiasi cha kumwandama Uhuru kwa sababu atapoteza zaidi kuliko kufaidika,” Profesa Manyora alisema kwenye mahojiano moja mapema wiki hii.
Anasema kwamba masuala ya kuandama familia ya Kenyatta kwa dai la kukwepa kulipa ushuru ni hewa kwa kuwa kuna sheria inayopaswa kufuatwa na sio kauli za kisiasa.
“Yeyote akiamua kumwandama na kumtesa Uhuru atakuwa akialika ghasia nchini,” alionya.
Baadhi ya wadadisi wanasema kwamba Uhuru ana nguvu nyingi kimataifa hata kama Ruto atamtoa pumzi nchini.
“Rais mstaafu ana nguvu nyingi ulimwenguni. Akiungana na Raila wanadhibiti asilimia 80 ya mitandao ya umaarufu,” asema Wakili Danstan Omari.
Mchanganuzi wa siasa Mutahi Ngunyi anasema ingawa Uhuru alitofautiana na Ruto wakiwa katika Jubilee, kiongozi wa nchi anaonyesha udhaifu kwa kulipiza kisasi.
“Ukweli usemwe, Uhuru alikukosea, lakini kuwa na kisasi ni udhaifu. Kisasi kinaweza kukuharibia mambo,” Bw Ngunyi alisema.
Inasemekana kuwa Rais Ruto alihakikishia wabunge wa Jubilee aliokutana nao Jumatano wiki hii kwamba hawezi kumkosea heshima mtangulizi wake Uhuru Kenyatta na familia yake, lakini akasisitiza ni sharti kila mtu alipe kodi.
Subscribe our newsletter to stay updated