NA CHARLES WASONGA
SERIKALI itatumia Sh489 milioni zaidi, kila mwaka, kugharamia mishahara ya maafisaa wakuu wa serikali ikiwa Rais William Ruto atawateua Mawaziri Wasaidizi (CASs) baada ya Mahakama ya Leba kutupilia kesi ya kupinga uteuzi wa maafisa hao.
Hii ni baada ya kubainika kuwa huenda Dkt Ruto atateua watu 22 kushikilia nyadhifa hizi wengi wao wakiwa wanasiasa waliowania viti mbalimbali katika uchaguzi mkuu uliopita na wakashindwa.
Watatwikwa wajibu wa kuwasaidia mawaziri katika utekelezaji wa majukumu ya afisi zao kama ilivyokuwa wakati muhula wa pili wa utawala wa Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta.
Kulingana na gredi za vyeo katika Tume ya Utumishi wa Umma (PSC) CASs wameorodheshwa katika gredi ya CSG3, sawa na daraja la kazi la V.
Hii ina maana kuwa kila mmoja wa maafisa hawa atapokea mshahara ya Sh765,188 kila mwezi.
Kando na hayo watapata marupurupu sawa na yale ambayo Mawaziri wanapokea japo wanawajibika kwa mawaziri hao.
PSC pia inaiorodhesha cheo cha CAS kuwa juu ya kile cha Katibu wa Wizara (PS) ambao kulingana na Agizo la Rais nambari 1 ya 2023, husimamia Idara mbalimbali katika Wizara za Serikali.
Wadadisi wa masuala ya siasa za uongozi wanasema kwa kuteua mawaziri wasaidizi, Rais Ruto atakuwa anafuata nyayo za Bw Kenyatta ya kuwatunuku wandani wake wa kisiasa kwa vyeo ambavyo, kimsingi, sio lazima vibuniwe.
Hatua hii, wanasema, ni sawa na kuwabebesha wananchi mzigo wa mkubwa kwani mishahara yao italipwa kwa pesa za umma ambazo ni ushuru unaotozwa wananchi.
Kulingana na data ya hivi punde kutoka kwa Benki Kuu ya Kenya (CBK) kiwango cha pesa ambazo serikali hutumia kulipa mishahara ya watumishi wa umma ilipanda kwa kima cha asilimia 5.5 hadi kufikia 520.03 bilioni mnamo Juni, 2022. Hili ni ongezeko la Sh27 bilioni kutoka Sh493 bilioni kufikia Juni, 2021.
Mzigo wa ulipigaji mishahara ya watumishi wa umma itarajiwa kupanda zaidi kufukia Juni mwaka huu, baada ya kuteuliwa CASs kwani Rais Ruto tayari amejitokeza kama kiongozi anayeongozwa na haja ya kuwazawadi wandani wake wa kisiasa.
Hii ni kinyume kabisa na msimamo wake alipokuwa akiendesha kampeni ya kusaka kura kutoka kwa wananchi kulielekea uchaguzi mkuu wa Agosti 9, 2022, ambapo Dkt Ruto alishikilia kuwa nia yake haikuwa kuunda serikali itakayowapa wanasiasa vyeo vikubwa, bali ile ambayo itaelekeza fedha nyingi za umma katika mipango na miradi ya kufaidi walala hoi, almaarufu mahasla.
Ni kwa misingi hii, ambapo Rais Ruto (wakati huo akiwa Naibu Rais), alipinga mchakato wa marekebisho ya Katiba kupitia mpango wa maridhiano (BBI) ulioungwa mkono na Bw Kenyatta pamoja na kiongozi wa Azimio Raila Odinga.
Miongoni mwa wandani wa Rais Ruto ambao inatarajiwa kuwa watateuliwa kushikilia nyadhifa za CASs ni pamoja na aliyekuwa Seneta wa Kakamega Cleophas Malala, aliyekuwa Gavana wa Migori Okoth Obado, alikuwa Seneta wa Mombasa Hassan Omar Sarai, aliyekuwa Naibu Gavana wa Kisii Joas Maangi, aliyekuwa Seneta Maalum Millicent Omanga na aliyekuwa Waziri wa Michezo Rashid Echesa.
Wengine ni wabunge wa zamani; Charles Kanyi Njagua (Starehe), Caleb Kositany (Soy), Benjamin Washiali (Mumias Mashariki), Cornelly Serem (Aldai), Chris Wamalwa (Kiminini), Tecla Tum (kaunti ya Nandi), Cate Waruguru (Laikipia), Moses Lessonet (Eldama Ravine), Joseph Limo (Kipkelion Mashariki), Purity Ngirici (Kirinyaga), miongoni mwa wengine.
Kuingana na PSC jumla ya Wakenya 5,000 walituma maombi mwaka 2022 walitaka wateuliwe nyadhifa za CASs, japo Rais Ruto anatarajiwa kuteua watu 22 pekee.
“Baada ya kesi ilipinga shughuli ya uteuzi wa maafisa hawa kutupa, sasa bodi ya PSC itakutana wiki ijayo kuchambua majina ya waliotuma maombi kisha kuorodhesha wale ambao wataalikwa kwa usaili,” akasema Mkurugenzi wa Mawasiliano ya PSC Browne Kutswa.
Bw Barasa Nyukuri ambaye ni mtaalamu wa masuala ya uongozi anasema kuwa kwa kuteua mawaziri wasaidizi Rais Ruto anakwenda kinyume cha sera yake mwenyewe ya kupunguza gharama ya matumizi ya serikali.
“Aidha, Dkt Ruto anaenda kinyume na ushauri wa Shirika la Fedha Ulimwenguni (IMF) kwamba serikali ipunguze gharama zisizo za dharura pamoja na gharama ya mishahara ya watumishi wa umma,” anasema.
Itakumbukwa kwamba, shirika hilo lilipotoa mkopo wa Sh261 bilioni kwa Kenya, mojawapo kati ya masharti lililoiwekea Kenya ni kupunguza mzigo wa ulipaji mishahara ili kuelekeza fedha nyingi katika miradi na mipango ya kuchochea ukuaji wa kiuchumi.
Subscribe our newsletter to stay updated