JUNGU KUU: Mipasuko yadhihirika katika Kenya Kwanza
NA BENSON MATHEKA
UASI wa muungano wa Azimio la Umoja One Kenya dhidi ya serikali na wito wa kuvunjwa kwa vyama tanzu vya Kenya Kwanza umefichua tofauti za ndani katika muungano huo tawala.
Muungano wa Kenya Kwanza unaoshirikisha vyama kadhaa vikiwemo United Democratic Alliance (UDA), Ford Kenya, United Democratic Movement (UDM), Maendeleo Chap Chap na Pamoja African Alliance (PAA) unaweza kutikiswa na misimamo tofauti ya vinara wake kuhusu jinsi ya kukabili uasi wa Azimio dhidi ya serikali ambao dalili zinaonyesha umeanza kushika kasi.
Vile vile, baadhi ya vyama tanzu vya Kenya Kwanza vimetofautiana kuhusu wito wa Katibu Mkuu wa United Democratic Alliance (UDA) Cleophas Malala vimezwe na chama hicho cha Rais William Ruto hatua inayoweka Kenya Kwanza kwenye hali tete kabla ya kumaliza mwaka mmoja uongozini.
Wito wa Bw Malala umepingwa vikali na chama cha Amani National Congress kilichoanzishwa na Mkuu wa Mawaziri Musalia Mudavadi ambaye alibanduka katika uongozi wake miezi michache iliyopita baada ya kuteuliwa serikalini.
Viongozi wa sasa wa chama hicho, wakiongozwa na Gavana wa Lamu Issa Timamy wamekataa wito wa Bw Malala, msimamo ambao ni sawa na wa chama cha Ford Kenya kinachoongozwa na Spika wa Bunge la Kitaifa Bw Moses Wetang’ula na Maendeleo Chap Chap cha Waziri wa Mashauri ya Kigeni Alfred Mutua.
Wadadisi wa siasa wanasema kwamba shinikizo za Bw Malala zinaonyesha kuwa kuna mzozo unaotokota kichini chini ndani ya Kenya Kwanza ambao unaweza kulipuka iwapo hautazimwa.
“Tunachoshuhudia ni mzozo unaogeuka kuwa vitisho tunavyoona kutoka kwa Bw Malala kwa vyama tanzu vya Kenya Kwanza. Hii inaweka muungano huo katika hali tete sana ikizingatiwa kuwa Bw Malala ni kipaza sauti cha kiongozi wa UDA ambaye ni Rais William Ruto ambaye anaonekana kuzima ushindani wa ndani akijiandaa mapema kwa uchaguzi mkuu wa 2027,” asema mchambuzi wa siasa Dkt Isaac Gichuki.
Anasema hatua ya Bw Malala inaonyesha kuna kiwango fulani cha vitisho ndani ya Kenya Kwanza hasa baada ya madai kwamba Dkt Mutua alipokonywa majukumu muhimu ya wizara yake baada ya kukataa kuvunja chama chake. Mapema mwezi huu majukumu muhimu ya wizara ya Mashauri ya Kigeni yalihamishiwa Afisi ya Bw Gachagua.
Kulingana na Katibu Mkuu wa Maendeleo Chap Mwengi Mutuse amepuuza shinikizo za Bw Malala huku ikiibuka kuwa viongozi wa vyama tanzu vya Kenya Kwanza walio serikalini wanatumia wandani wao kumjibu seneta huyo wa pili wa Kaunti ya Kakamega. Wadadisi wa siasa wanasema kwamba kutofautiana kwa Bw Mudavadi na Rais William Ruto na Naibu Rais Rigathi Gachagua kuhusu jinsi ya kushughulikia uasi wa Azimio ni dalili za mgawanyiko na mtihani kwa uthabiti wa muungano tawala.
Huku Rais Ruto na Bw Gachagua wakishikilia kuwa hawatazungumza na upinzani, Bw Mudavadi anasema njia ya pekee ya kujenga nchi ni kukumbatia mazungumzo kwa nia njema kisiasa.
Bw Gichuki anasema kauli ya Bw Mudavadi alipokuwa akizungumza katika hafla ya Kituo cha Demokrasia ya Vyama Vingi mnamo Alhamisi wiki hii, inaonyesha viongozi wakuu serikalini wamegawanyika kuhusiana na uasi unaoendelezwa na upinzani hasa kwa kuwa Ruto ameapa hatazungumza na upinzani na kupuuza matakwa yao.
Bw Mudavadi ni kiongozi wa tatu kwa ukubwa katika mpangilio wa serikali ya Kenya kwanza na kuwa na msimamo tofauti na wakubwa wake kunatoa taswira ya hali tete katika muungano wa Kenya Kwanza.
Next article
Patashika EPL Arsenal, Man-U wakisaka ubabe