NA WANDERI KAMAU
MASAIBU yanayomkumba Gavana Kawira Mwangaza wa Meru, yamefungua ukurasa mpya kuhusu mivutano ambayo imekuwepo kati ya magavana na madiwani tangu kuanzishwa kwa mfumo wa ugatuzi 2013.
Kwa mujibu wa wadadisi wa siasa, ni hali ambayo pia itaonyesha mikakati atakayoweka Rais William Ruto kusuluhisha mivutano itakayoibuka katika serikali za kaunti, ikitarajiwa kwamba atawategemea sana magavana kumsaidia kutimiza baadhi ya ahadi alizotoa kwa Wakenya.
Tangu kuapishwa kuwa Rais, Dkt Ruto amesisitiza kuwa atawategemea sana magavana kutekeleza baadhi ya masuala muhimu kama kilimo, kulainisha sekta ya afya, ujenzi wa miundomsingi, kati ya masuala mengine.
Mzozo katika kaunti hiyo ulianza wiki iliyopita, madiwani wakimlaumu Bi Mwangaza kwa kuwatenga na kuwa “mwenye kiburi.”
Kiongozi wa Wengi katika Bunge la Kaunti, Bw Evans Mawira, alisema imekuwa vigumu kumfikia gavana huyo, licha ya sheria kuhitaji magavana na madiwani kushirikiana katika utekelezaji wa baadhi ya majukumu kama vile upitishaji wa bajeti.
“Lazima gavana afahamu kuwa madiwani pia ni viongozi waliochaguliwa na wananchi, hivyo lazima awasikilize,” akasema Bw Mawira.
Hata hivyo, kwa mujibu wa Bw Javas Bigambo, aliye mchanganuzi wa siasa na masuala ya uongozi, mvutano huo mpya utakuwa kibarua kipya kwa utawala wa Kenya Kwanza kuhusu mikakati utakayoweka katika kushirikiana na serikali za kaunti.
“Kwa mwezi mmoja uliopita, Rais Ruto na naibu wake Rigathi Gachagua wamefanya mikutano mingi na magavana, hatua inayoonyesha jinsi kaunti zitakuwa muhimu kuwawezesha kutekeleza ajenda yao,” akasema Bw Bigambo.
Mdadisi huyo asema kuwa ili kuhakikisha jahazi lao la kisiasa halizami, Rais Ruto na Bw Gachagua wanafaa kuingilia kati na kusuluhisha mzozo huo kabla ya kutokota.
Katika uchaguzi wa 2013, hakuna mwanamke hata mmoja aliyechaguliwa kuwa gavana.
Hali ilibadilika mnamo 2017, baada ya wanawake watatu kuchaguliwa kuwa magavana. Watatu hao ni Bi Anne Waiguru (Kirinyaga), Charity Ngilu (Kitui) na marehemu Joyce Laboso (Bomet).
Idadi hiyo iliongezeka na kufikia magavana saba kwenye uchaguzi wa Agosti 9.
Wanasiasa kadhaa kutoka eneo la Mlima Kenya Mashariki waliozungumza na ‘Jamvi la Siasa’ wanasema itamlazimu Rais Ruto na Bw Gachagua kuingilia mzozo wa Meru, kwani kaunti hiyo ni miongoni mwa maeneo yaliyowapigia kura nyingi zaidi kwenye uchaguzi wa mwaka huu.
Miongoni mwa ahadi alizotoa Rais Ruto ni kutafuta masoko zaidi ya kimataifa kwa zao la miraa, kwani ndilo kitegauchumi kwa wakazi wengi katika eneo hilo.
“Maelfu ya watu katika eneo la Meru na Mlima Kenya kwa jumla walimpigia kura Rais Ruto kwa ahadi ya kuboresha kilimo cha miraa, kahawa, majanichai na ufugaji. Kilimo kikiwa moja ya sekta zinazosimamiwa na serikali za kaunti, Dkt Ruto hana jingine ila kufanya kila awezalo kusuluhisha mzozo huo,” asema Bw Kipkorir Mutai, ambaye ni mchanganuzi wa siasa.
Wadadisi wanasema ikiwa Rais Ruto atafaulu kuudhibiti mzozo huo, basi itaashiria kwamba hatakuwa na mazingira magumu kutimiza ahadi zake.
Bi Mwangaza anamlaumu Naibu Spika wa Seneti Kathuri Murungi kati ya vigogo wengine wa kisiasa kuwa chanzo cha masaibu yanayomwandama.
Subscribe our newsletter to stay updated