• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 3:03 PM
KAMAU: Kenya iziige nchi nyingine duniani kulinda tamaduni zake

KAMAU: Kenya iziige nchi nyingine duniani kulinda tamaduni zake

Na WANDERI KAMAU

MOJA ya changamoto kuu zinazokikumba kizazi cha sasa nchini ni ukosefu wa ufahamu wa lugha zao asili.

Ingawa lugha hizo humpa mtu utambulisho halisi kuhusu asili yake, inashangaza kwamba kizazi hicho kinazichukulia kama njia za “kujidunisha.”

Dhana hiyo ndiyo imejenga mtindo mpya ambapo kinyume na malezi ya awali, watoto wanalelewa kwa kulazimishwa kujifunza na kukifahamu Kiingereza pekee.

Katika mazingira hayo ya “usasa”, Kiswahili pia kinachukuliwa kuwa lugha duni! Naam, kinaonekana kuwa lugha ya watu ambao hawakuelimika, wazee na “wasioufahamu usasa.”

Binafsi, huenda fasiri yangu ya “usasa” ikakinzana na uelewa wa watu wengi.

Hata hivyo, ni wazi kuwa usasa haumaanishi jamii kusahau misingi yake ya kimaisha na utamaduni wake.

Kote duniani, kila jamii inapitia mabadiliko makubwa ya mitindo yake ya kimaisha kutokana na masuala kama mpenyo wa kiteknolojia.

Kinyume na zamani, jamii nyingi zinaendesha maisha yake kutokana na mazingira yanayosukumwa na usasa katika karibu kila nyanja.

Hivyo, ni hali isiyoepukika hata kidogo.Hata hivyo, kinyume na hali ilivyo nchini, jamii nyingi duniani zinaendelea kulinda misingi yake ya kitamaduni na kimaisha.

Kinaya ni kuwa, nyingi za jamii hizo zipo katika nchi zinazoonekana kuukumbatia usasa kwa kiasi kikubwa.

Kwa mfano, katika mataifa kama Ujerumani, lugha yao asili hadi sasa ni Kijerumani. Ni makosa kwa mtoto yeyote kukua bila kuifahamu lugha hiyo.

Kulingana na mtaala wa elimu nchini humo, Kijerumani huwa miongoni mwa masomo ya msingi ambayo kando na kuwa lugha ya msingi ya mawasiliano, mwanafunzi huwa anatahiniwa katika kila kiwango cha elimu.

Mtindo uo huo ndio unaoendelezwa katika nchi kama Norway, Ubelgiji, Ufaransa, Ureno, Uhispania kati ya nyingine.

Hapa Afrika, baadhi ya mataifa yanayoonekana kuweka juhudi kulinda lugha zake asili ni Rwanda, Burundi na Tanzania.

Nchini Rwanda, ni lazima wanafunzi katika viwango vya shule ya msingi na upili wajifunze Kinyarwanda. Katika baadhi ya taasisi, lugha hiyo huwa miongoni mwa masomo ambayo hutahiniwa katika kiwango cha kitaifa.

Vivyo hivyo, imefika wakati kwa Kenya kuyaiga mataifa mengine kwenye juhudi za kuweka msingi wa kulinda mitindo yake ya kimaisha na kitamaduni.

Kujivika ‘usasa’ ni njia ya kukipotosha na kukipoteza kizazi kilichopo. Lazima tuweke msingi bora kuhakikisha tunaendeleza tamaduni zetu bila kusombwa na usasa.

[email protected]

You can share this post!

TAHARIRI: Hakuna raha tena kushabikia Stars

MUTUA: Mwafrika amejihini na kujitweza mwenyewe