• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
KAMAU: Tamaa imegeuza Afrika kuwa ‘soko la utumwa’

KAMAU: Tamaa imegeuza Afrika kuwa ‘soko la utumwa’

Na WANDERI KAMAU

UFICHUZI wa sakata ambapo watu maarufu duniani wamekuwa wakificha mabilioni ya fedha katika akaunti za siri ng’ambo umeibua kinaya kilichopo kuhusu maana halisi ya “uhuru” barani Afrika.

Miongoni mwa watu waliotajwa kwenye ufichuzi huo ni viongozi maarufu, wanaosifika kwa kuwa “mashujaa wa ukombozi” katika nchi zao.

Kando na familia ya Mzee Jomo Kenyatta, viongozi wengine waliotajwa kuwa na akaunti za siri ughaibuni ni marais Ali Bongo (Gabon), Dennis Sassou Nguesso (Congo Brazaville) kati ya wengine.

Aliyetajwa pakubwa kwenye familia ya Mzee Kenyatta ni Rais Uhuru Kenyatta, ikizingatiwa ana umaarufu mkubwa kutokana na nafasi anayoshikilia kama rais wa Kenya.

Ingawa ufichuzi haumaanishi viongozi hao walipora fedha hizo kutoka nchi zao, kinaya ni kuwa umedhihirisha watu maskini wataendelea kuteseka katika lindi lao, huku matajiri wakizidi kuogelea katika bahari ya mamilioni ya pesa.

Lengo kuu la vita vya ukombozi katika nchi nyingi za Afrika lilikuwa kuondoa hali ambapo pengo kati ya watu maskini na matajiri liliendelea kupanuka.

Haya ndiyo maovu yaliyowakasirisha vikali Waafrika kiasi cha kuanza vita vikali kujikomboa dhidi ya udhalimu wa wakoloni.

Hata hivyo, tathmini ya matukio ambayo yameendelea katika bara hili kwa nusu karne iliyopita, yanaonyesha pengine wakati haukuwa umefika kwa wakoloni kuondoka.Kwa miaka 50 iliyopita, Afrika imebaki kama kigae.

Taswira yake imedorora.

Sekta muhimu za kiuchumi zimevurugika kutokana na utawala mbaya wa mataifa hayo.

Ni wazi kuwa hali barani humu imeathirika vibaya kuliko ilivyokuwa chini ya wakoloni.Kwa mfano, licha ya Kenya kuwa chini ya utawala wa Waingereza kati ya 1895 na 1963, hakuna wakati ambapo kuliwahi kuripotiwa baa la njaa.

Wakati huo, kila jamii ilikuwa ikijitosheleza kwa chakula bila matatizo yoyote. Hii ni licha ya jamii nyingi kuishi kwa kuambatana na mtindo wa maisha ya kikale.

Nyakati hizo ilikuwa nadra kusikia kuna chimbuko au mkurupuko wa maradhi hatari kama vile saratani, malaria au virusi vya corona.

Watu walikuwa wenye afya.

Hakukuwa na hospitali nyingi sababu wanajamii walikuwa wakila vyakula asili.Maisha yalikuwa shwari licha ya uwepo wa ukatili, dhuluma na mateso ya wakoloni.

Lakini hali iligeuka baada ya Waafrika kuchukua uongozi wa nchi zao.

Matumaini yaliyokuwepo yalibadilika kuwa vilio na majonzi yasiyoisha. Matumaini ya wananchi yakawa huzuni tupu.

Je, asili ya mahangaiko hayo ni ipi?

Ingawa wakoloni walikuwa wakatili dhidi ya Waafrika, walihakikisha wamepata mahitaji yao ya msingi kama vile chakula, mavazi na malazi.

Ukatili wao haukupita mipaka ya kushusha hadhi yao ya kibinadamu – kama kupora mali na kuielekeza kwa jamaa na familia zao pekee bila kujali hali za raia wengine.

Viongozi wa Kiafrika – maarufu kama Wakoloni Weusi – walipora kila kitu ili kufaidi familia zao huku mamilioni ya raia wakiumia.Hilo ndilo limeligeuza bara hili kuwa ‘Soko la Kisasa la Utumwa’.

Hatujajikomboa hata kidogo.

[email protected]

You can share this post!

Sutton athubutu kusema Salah anapiku Ronaldo na Messi...

Mlipuko wa ugonjwa wa kuhara wazua hofu vijijini Boni