NA PHILIP MUYANGA
BAADA ya Mahakama Kuu kuthibitisha kuchaguliwa kwa Bi Fatuma Achani kama gavana wa Kwale maoni tofauti tofauti yalitolewa kulingana na uamuzi huo.
Wafuasi wa Bi Achani waliusifu uamuzi huo huku wakisema wakati wa siasa ulikuwa umekwisha na lililosalia lilikuwa ni viongozi kuwafanyia wananchi kazi.
Baadhi ya wafuasi wa wapinzani wa gavana huo walionekana kutoridhishwa na uamuzi wa mhakama inagawa walisema wanauheshimu.
Kwa sasa swali wananchi wengi wanajiuliza ni iwapo viongozi wa kaunti ya Kwale wataungana na kuweka tofauti zao za kisiasa kando na kuamua kuwafanyia kazi wakaazi wa kaunti hiyo.
Baadhi ya wakaazi wa kaunti hiyo wanasema kuwa viongozi wao wanafaa kuungana na kutekeleza majukumu yao ambayo ni ya manufaa kwa mwananchi hususan yule wa kipato cha chini.
Kwa muda mrefu sasa wachanganuzi wa siasa za Pwani wanasema kuwa kutoshirikiana baina ya viongozi wa kaunti za ukanda wa Pwani kunaleta ukosefu wa maendeleo na kunawagawanya wananchi kwa mirengo tofauti ya kisiasa badala ya kuwaunganisha kimaendeleo.
Baadhi ya wachanganuzi wa siasa wanasema kuwa kwa sasa viongozi wa kaunti ya Kwale ni sharti wafanye kazi kwa pamoja na kuhakikisha ya kuwa suala la utoaji wa huduma kwa wananchi ndio linapewa kipao mbele.
Ushirikiano
Hata hivyo,wanaongeza kusema kuwa ushirikiano baina ya Bi Achani na viongozi wengine hakumaanishi ya kuwa gavana huyo hatakosolewa iwapo hatafanya makosa kwani hilo ndilo jukumu lao pia.
Baada ya kutangazwa mshindi wakati kura zilipomalizwa kuhesabiwa, Bi Achani alikuwa ameonekana kuwa tayari kukabiliana na wapinzani wake mahakamani huku akisema kuwa hawafai kuweka taharuki yeyote.
Hata hivyo baada ya Jaji Francis Gikonyo kutoa uamuzi wake kuhusiana na kesi yakupinga kuchaguliwa kwake,Bi Achani alionekana mtulivu na kusema kuwa yuko tayari kufanya kazi na wapinzani wake.
“Natakaka kuwaambia wapinzani wangu kuwa mama anaweza,wakuje mezani tuendeleze Kwale niko tayari kufanya kazi na mtu yeyote kwa ajili ya Mkwale,” alisema Bi Achani.
Aliongeza kusema kuwa kazi ameifanya na kwamba ataendelea kuifanya na kwamba waliokuwa wamefika mahakamani walikuwa wakitekeleza haki yao na wala yeye hakuwa na wasiwasi wowote kuhusiana na kesi hiyo.
Msimamo wake ulionekana kuugwa mkono na naibu wake Bw Chirema Kombo aliyesema kuwa watafanya kazi kwa ajili ya wananchi wa Kwale bila ubaguzi wowote.
Bi Achani alishinda ugavana wa kaunti ya Kwale kwa kura 59,674 huku Prof Hamadi Boga akifuata na kura 53,972, Lung’azi Mangale 47,639 na Bw Chirau Ali Mwakwere 9,639.
Prof Halimu Shauri ambaye ni mchanganuzi wa siasa alisema kuwa Bi Achani kuwaita wapinzani wake kufanya kazi pamoja ni maneno tu ya uhusiano mwema.
“Suala la kwanza la kuwaita wapinzani wako mfanye nao kazi ni kuwa je ajenda ya kuwaita ni nini? hatuajaona akiwa na ajenda ya kuwaita watu wakae na kujadili masuala ya kaunti,” alisema Prof Shauri ambaye pia ni mhadhiri wa chuo kikuu cha Pwani kaunti ya Kilifi.
Prof Shauri alisema kuwa Bi Achani anafaa kuonyesha kuwa yuko tayari kufanya kazi na wapinzani wake.
Ajenda
Kulingana na mchanganuzi huyo wa siasa, Bi Achani pia anafaa kuweka ajenda ambayo inahusisha kila mtu na itakayohitaji wapinzani wake wa kisiasa kukaa naye na kujadiliana masuala ya kaunti ya Kwale.
“Na sio wapinzani wake tu, ni ajaribu pia kuitisha mkutano na wasomi wa kaunti ya Kwale kama vile madaktari na wahandisi ili wajadiliane mambo muhimu ya kaunti hata kabla hajawaita wapinzani wake,” alisema Prof Shauri.
Katika uamuzi wake wiki iliyopita, Jaji Francis Gikonyo alisema kuwa hakukuwa na ushahidi wowote ya kuwa uchaguzi wa Bi Achani ulikuwa na dosari zozote au haukufuata sheria za uchaguzi na katiba kwa upande wa tume ya uchaguzi na mipaka nchni (IEBC).
Jaji huyo alisema kuwa Bi Achani alichaguliwa kihalali katika uchaguzi huo wa Agosti 9, 2022 na kwamba baada ya kuangalia ushahidi uliowasilishwa mahakamani hakuona sababu yeyote ya kufutilia mbali ushindi huo wa gavana.
Aliongeza kusema kuwa madai ya hongo na vitendo vya makosa ya uchaguzi hayakuthibitishwa na waweka kesi.
Katika kesi hiyo, Bw Dziwe Pala na mwenzake Suleiman Ali walikuwa wanataka ushindi wa Bi Achani ufutiliwe mbali kwa madai ya makosa ya uchaguzi.
Mchanganuzi mwingine wa masuala ya siasa Bw Ayub Mwangi alisema kuwa wapinzani wa Bi Achani wanaweza kuamua kufanya kazi naye au kumpinga wakati wa muhula wake wa uongozi.
Bw Mwangi ambaye pia ni mtaalum katika masuala ya mawasiliano alisema kuwa wale watakaomuunga gavana huyo mkono wanaweza kufaidika kisiasa.
“Wale watakaoamua kufanya kazi na gavana kuna uwezekano wa kufaidika kisiasa huku wapinzani wakitolewa kisiasa na kutokuwa na ushawishi wowote,” alisema Bw Mwangi.
Mwanasiasa mkongwe wa Mombasa Bw Abdulrahman Abdalla alisema kuwa ni muhimu sana kwa viongozi wa kaunti ya Kwale kufanya kazi kwa pamoja kwani baada ya uamuzi wa mahakama siasa huwa zimekwisha.
“Tukitaka kuendeleza ukanda wa Pwani ni lazima viongozi wa kaunti waungane na kwenda mbele pamoja kwa manufaa ya wakaazi,” alisema Bw Abdalla.
Aliongeza kusema kuwa uchaguzi wa ugavana kaunti ya Kwale ulikuwa umeisha na kwamba baaada ya mahakama kutoa uamuzi wake,ni vyema wananchi wapate huduma bora,” alisema Bw Abdalla.
Subscribe our newsletter to stay updated